Ardhi ya Ikulu imenyakuliwa na watu binafsi, Bunge laambiwa
MSIMAMIZI wa Ikulu Katoo Ole Metito, amefichua kuwa sehemu kubwa ya ardhi inayomilikiwa na Ikulu na Ikulu Ndogo nchini imenyakuliwa huku wabunge wakitaka hatua za haraka zichukuliwe kuirejesha.
Akizungumza bungeni wakati wa majadiliano kuhusu Sera ya Bajeti 2026 (BPS), Ole Metito alisema serikali inapanga kutumia Sh1.03 bilioni katika ukarabati wa Ikulu na Ikulu Ndogo katika mwaka ujao wa kifedha.
Aliongeza kuwa Ikulu inaendelea kutoa msaada wa kimkakati kwa Rais katika utekelezaji wa majukumu yake ya kikatiba pamoja na kuendeleza ajenda ya mabadiliko ya serikali.
Kiongozi wa Kamati, Gabriel Tongoyo (Narok Magharibi), aliitaka serikali kuchukua hatua za haraka kurejesha ardhi hiyo.
Ole Metito alisema ekari 100 za ardhi ya Ikulu Ndogo ya Kakamega ambazo ziliwahi kunyakuliwa tayari zimerudishwa.
Hata hivyo, alisema zilizoathiriwa zaidi na unyakuzi wa ardhi ni Ikulu Ndogo za Kisumu, Nakuru na Eldoret.