Habari

Wakenya wengi bado wanalemewa na gharama ya maisha licha ya maandamano ya Gen Z

Na CONSTANT MUNDA NA JOHN MUTUA June 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MIAKA miwili baada ya maandamano ya vijana wa Gen Z yaliyotikisa taifa ya kupinga Mswada wa Fedha wa 2024, Wakenya wengi bado wanakabiliwa na changamoto zilezile za kiuchumi zilizowasukuma kuingia barabarani.

Ingawa baadhi ya mapendekezo ya ushuru yaliyokuwa kwenye mswada huo yaliondolewa kufuatia maandamano hayo, gharama ya maisha imeendelea kupanda na kulazimisha familia nyingi kubadili jinsi zinavyotumia mapato yao.

Takwimu za Shirika la Kitaifa la KNBS zinaonyesha kuwa wastani wa mapato halisi ya kila mwezi uliongezeka kutoka Sh55,452 mwezi Juni 2024 hadi Sh56,566 mwezi Juni 2025.

Hata hivyo, kiwango hicho bado kiko chini kwa zaidi ya Sh3,300 ikilinganishwa na Sh59,895 zilizorekodiwa mwaka 2021, jambo linaloonyesha kuwa uwezo wa ununuzi haujarejea katika kiwango cha miaka minne iliyopita.

Kwa mujibu wa takwimu hizo, familia nyingi sasa zinatumia sehemu kubwa ya mapato yao kununua chakula na kugharamia usafiri huku zikibana matumizi ya mavazi, burudani na bidhaa nyingine zisizo za lazima.

Mfumuko wa bei za chakula ulipanda kutoka asilimia 6.2 mwezi Mei 2024 hadi asilimia 9.4 mwezi Mei 2026.
Wakati huo huo, gharama za usafiri ziliongezeka kwa asilimia 16.5, huku kiwango cha jumla cha mfumuko wa bei kikifikia asilimia 6.7 kutoka asilimia 5.1.
Hali hiyo imefanya familia nyingi zitumie fedha nyingi zaidi ili kudumisha maisha yale yale ya kawaida.

Akisoma Bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 mnamo Juni 11, Waziri wa Fedha, John Mbadi alikiri kuwa malalamishi makuu yaliyotolewa na wananchi katika mikutano ya mashauriano yalihusu gharama ya maisha.

“Ujumbe kutoka kwa Wakenya ni wazi. Wanataka uchumi unaowafaa, gharama nafuu ya maisha, nafasi zaidi za ajira na biashara pamoja na matunda ya ukuaji wa uchumi kuwafikia wananchi wote,” alisema Mbadi.

Aliongeza kuwa wananchi pia walitaka ushuru wa bidhaa muhimu upunguzwe, matumizi mabaya ya fedha za umma yadhibitiwe na vita dhidi ya ufisadi viimarishwe.
Kauli hizo zinaakisi malalamishi yaliyokuwa kiini cha maandamano ya Gen Z mwaka 2024.

Kwa Amos Kwedho, mfanyakazi eneo la mashambani, hali ya uchumi bado ni ngumu.

“Hali ilivyo mashinani ni tofauti na jinsi serikali inavyoelezea. Uwezo wa watu kutumia fedha umeshuka sana tangu mwaka 2024. Watu wengi hawana pesa mifukoni na kama hujashindwa kulipa deni lako, mshukuru Mungu,” alisema.

Kwedho alisema alilazimika kufunga biashara yake ya pikipiki za boda boda mwaka jana baada ya wahudumu kushindwa kulipa ada ya kila siku kutokana na kupanda kwa bei ya mafuta na vipuri.

Aliuza pikipiki zake 10 na kuwekeza fedha hizo katika baa yake, lakini hata biashara hiyo imeathiriwa kwa sababu wateja hawatumii fedha kama awali.
Kwa mujibu wake, faida ya biashara hiyo imepungua kwa karibu asilimia 20 ikilinganishwa na mwaka 2022.

Mbali na kupanda kwa bei ya chakula, mafuta pia yameendelea kuwa mzigo mkubwa kwa wananchi. Bei ya lita moja ya dizeli imeongezeka kwa Sh49.76 katika kipindi cha miaka miwili na kufikia Sh232.86 jijini Nairobi, huku petroli ikipanda kwa Sh24.19 hadi Sh214.25 kwa lita.