Utumishi Girls: Wanafunzi 8 kupimwa akili kabla ya kujibu mashtaka ya mauaji
MAHAKAMA Kuu ya Kibera imeahirisha kusomwa kwa mashtaka dhidi ya wanafunzi 8 wa Shule ya Upili ya Wasichana ya Utumishi Academy, Gilgil, hadi watakapofanyiwa uchunguzi wa afya ya akili na kuthibitishwa umri wao.
Mahakama ilisema Ijumaa kuwa hawawezi kujibu mashtaka 16 ya mauaji kabla ya kuthibitishwa kuwa wana uwezo wa kiakili wa kusimama kizimbani.
Wanafunzi hao wanalaumiwa kwa kuhusika na mkasa wa moto uliozuka katika bweni la shule hiyo Mei 28, 2026 na kusababisha vifo vya wanafunzi 16.
Mahakama pia ilisema washtakiwa wanahitaji kuwakilishwa na mawakili kwa kuwa kosa la mauaji chini ya Kifungu cha 203 kinachosomwa pamoja na Kifungu cha 204 cha Kanuni ya Adhabu linaweza kuadhibiwa kwa kifungo cha maisha au hukumu ya kifo.
Upande wa mashtaka ulieleza kuwa wanafunzi hao walifikishwa mahakamani ili kufahamishwa mashtaka yaliyoidhinishwa na Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP), wala si kujibu mashtaka hayo.
Jaji aliamuru wanafunzi hao, ambao wanazuiliwa katika Kituo cha Marekebisho cha Watoto cha Kabete, wafanyiwe uchunguzi wa afya ya akili mwishoni mwa wiki na pia wapimwe umri wao.
Aidha, aliagiza wazazi, walezi au mawakili wao waandamane nao mahakamani Julai 1, 2026, watakapotarajiwa kusomewa rasmi mashtaka na kujibu iwapo wana hatia au la.
Kesi hiyo ilihamishwa kutoka Mahakama ya Naivasha hadi Kibera kwa sababu za kiusalama kutokana na ukaribu wa mahakama ya awali na eneo ambalo mkasa ulitokea