Habari

Masharti mapya ya KCSE kwa waliokosa KCPE

June 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BARAZA la Kitaifa la Mitihani Kenya (KNEC) limetangaza masharti mapya yanayowahusu wanafunzi wanaotarajia kufanya mtihani wa kidato cha nne (KCSE) mwaka 2027 wasio na cheti cha Mtihani wa Darasa la Nane (KCPE).

KNEC imesema wanafunzi hao hawataruhusiwa kujisajili moja kwa moja kwa mtihani wa KCSE, bali watalazimika kwanza kuthibitisha sifa zao za elimu ya msingi na kufanya mtihani maalumu wa kufuzu.

Hatua hiyo itawahusu wanafunzi wote wasiokuwa na cheti cha KCPE au sifa zinazolingana nacho, wakiwemo waliokosa kufanya mtihani wa KCPE mwaka 2023 lakini wakaruhusiwa kujiunga na shule za upili kwa idhini ya Wizara ya Elimu.

Katika taarifa, KNEC ilisema wanafunzi hao lazima wawasilishe thibitisho kwamba walisoma shule ya msingi kabla ya kuruhusiwa kufanya mtihani wa kufuzu utakaofanyika Septemba 2026.

“Watu wote wasiokuwa na vyeti vya KCPE au sifa zinazolingana navyo wanaonuia kufanya KCSE mwaka 2027 watawasilisha sifa zao za elimu ya msingi kwa KNEC ili zithibitishwe, kisha wafanye mtihani wa kufuzu,” ilisema taarifa hiyo.

Mkurugenzi Mkuu wa KNEC, Dkt David Njengere, alisema KCSE ya mwaka 2027 itakuwa ya mwisho chini ya mfumo wa elimu wa 8-4-4, kabla ya Kenya kuhamia kikamilifu mfumo wa elimu inayotegemea umilisi (CBE) mwaka 2028.

Alisema wanafunzi waliowahi kuacha shule kabla ya kufanya KCPE au waliosajiliwa lakini hawakufanya mtihani huo wanapaswa kutumia nafasi hiyo ya mwisho.

“Tunapojiandaa kutekeleza kikamilifu mfumo wa CBE mwaka 2028, ni muhimu kwa yeyote ambaye hajakamilisha mahitaji chini ya mfumo wa 8-4-4 achukue fursa hii kufanya KCSE ya mwisho mwaka 2027. Nawasihi Wakenya wasisubiri hadi dakika za mwisho,” alisema Dkt Njengere.

KNEC imewaagiza wakuu wa shule kuhakikisha wanafunzi wote wa Kidato cha Tatu mwaka huu ambao hawana vyeti vya KCPE wanazingatia masharti hayo ndani ya muda uliowekwa.

Katika mchakato wa uthibitishaji, wanafunzi watahitajika kuwasilisha barua ya maombi, ripoti za maendeleo shuleni au nyaraka nyingine zinazoonyesha walisoma shule ya msingi. Pia watalipa ada ya Sh3,480 kwa uthibitishaji wa sifa zao.

Baada ya kukamilisha hatua hiyo na kuthibitishwa, watapewa barua ya kuwaruhusu kujiandikisha kwa mtihani wa kufuzu.

Usajili wa mtihani huo tayari umefunguliwa kupitia mfumo wa KNEC na utafungwa Julai 30, 2026. Watahiniwa pia watalipa Sh3,000 kupitia mfumo wa e-Citizen ili kufanya mtihani huo.

Mtihani huo utafanyika mtandaoni Septemba katika vituo vitakavyotambuliwa na Wakurugenzi wa Elimu wa Kaunti, huku makao makuu ya kaunti yakitarajiwa kutumika kama vituo vya mitihani.

Wanafunzi wa kawaida watahitajika kuwasilisha barua kutoka shuleni mwao, ilhali watahiniwa wa kujitegemea watawasilisha barua kutoka kwa Mkurugenzi wa Elimu wa eneo husika.

Pia watawasilisha picha ya pasipoti, cheti cha kuzaliwa au kitambulisho cha taifa, pamoja na barua ya KNEC ya kuidhinisha vyeti kwa wale waliosomea nje ya nchi.

KNEC ilisema mtihani huo pia utawahusu wanafunzi wenye vyeti vya elimu vya mataifa ya kigeni baada ya vyeti hivyo kuidhinishwa rasmi na baraza hilo.

Matokeo ya mtihani wa kufuzu ndiyo yatakayoamua iwapo mwanafunzi ataruhusiwa kujiandikisha kwa KCSE ya mwaka 2027.

Tangazo hilo linajiri huku Kenya ikijiandaa kuhitimisha mfumo wa elimu wa 8-4-4 uliodumu kwa takriban miongo minne. Mwaka huu, zaidi ya watahiniwa milioni 3.5 wamejiandikisha kufanya mitihani ya kitaifa ya KPSEA, KJSEA na KCSE, huku zaidi ya wanafunzi milioni moja wakisajiliwa kufanya KCSE kwa mara ya kwanza katika historia ya mtihani huo.

Kutokana na hali hiyo, KNEC inatarajia shule, wazazi na wanafunzi walioathiriwa kuharakisha mchakato wa kuthibitisha rekodi zao ili wasikose nafasi ya kufanya KCSE ya mwisho chini ya mfumo wa 8-4-4.