Vinara wa upinzani wahepa kampeni chaguzi ndogo nne zikifanyika kesho
WAPIGAKURA katika maeneo manne ya uchaguzi, kiti kimoja cha ubunge na viti vitatu vya wadi, wanatarajiwa kupiga kura leo katika chaguzi ndogo ambazo Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka imesema iko tayari kikamilifu kusimamia.
Kampeni za kiti cha ubunge cha Isiolo South na wadi ya West Kabras (Kaunti ya Kakamega), pamoja na wadi za Evurore na Muminji (Kaunti ya Embu), zilifungwa rasmi Jumatatu huku wagombea wakifanya juhudi za mwisho kuwashawishi wapigakura.
Katika kipindi chote cha kampeni, vinara wa upinzani hawakuonekana katika wadi hizo, hali iliyowaacha viongozi wa UDA wakipigia debe wagombea wao bila upinzani wa moja kwa moja kutoka kwa viongozi wakuu wa muungano wa upinzani.
Kutokuwepo kwao kumeibua mjadala miongoni mwa wakazi, baadhi wakihisi kuwa uchaguzi huo haukupewa uzito unaostahili na viongozi hao.
Kwa upande mwingine, Naibu Rais Kithure Kindiki alijitokeza mara kadhaa kushiriki katika kampeni, akiandamana na Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku, Gavana wa Embu Cecily Mbarire na Seneta Alexander Mundigi.
Viongozi hao waliwahimiza wakazi kuwachagua wagombea wa UDA ili kuimarisha ushirikiano kati ya serikali ya kaunti na ile ya kitaifa.
Viti vya Evurore na Muminji vilibaki wazi baada ya Duncan Mbui na Newton Kariuki kujiuzulu mwaka jana kuwania ubunge wa Mbeere North, lakini wakashindwa na mgombea wa United Democratic Alliance (UDA), Leonard Wa Muthende Njeru.
Kiti cha Isiolo South kilibaki wazi kufuatia kifo cha Mbunge Mohamed Bidu, huku kiti cha West Kabras kikibaki wazi baada ya David Ndakwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa Malava.
(IEBC imesema imekamilisha usambazaji wa vifaa vya uchaguzi, pamoja na kupima na kuandaa mashine za KIEMS kwa zoezi hilo.
Tume hiyo ilieleza kuwa maafisa wa uchaguzi wamepatiwa mafunzo kuhusu taaluma, uadilifu na taratibu sahihi za upigaji kura. Vituo vitafunguliwa saa kumi na mbili asubuhi na kufungwa saa kumi na moja jioni, huku wapigakura watakaokuwa kwenye foleni wakiruhusiwa kupiga kura hata baada ya muda wa kufunga.
Hata hivyo, tayari visa vya vurugu vimeripotiwa katika Kaunti ya Embu, ambako mfuasi wa chama cha Devolution Empowerment Party (DEP) alidungwa kisu na kuuawa wakati wa kampeni. Polisi wanasema uchunguzi unaendelea ili kubaini waliohusika.
Naibu Rais Kithure Kindiki aliwataka wakazi wa Isiolo na Mbeere North kudumisha amani wakati wa uchaguzi. Alieleza imani kuwa UDA itashinda viti vyote.
Katika kinyang’anyiro cha Isiolo South, Gavana Abdi Guyo, Seneta Fatuma Dullo, Mwakilishi wa Wanawake Mumina Bonaya na Spika Abdullahi Banticha wamekuwa wakimpigia debe mgombea wa UDA Mohamed Tubi. Tubi anakabiliana na dada yake mkubwa, Bina Mohamed wa Jubilee Party, huku wagombea wengine wawili pia wakiwania kiti hicho.
Katika wadi ya West Kabras, Elphas Shalakha wa UDA anamenyana na wagombea wa vyama mbalimbali akiwemo wa Orange Democratic Movement (ODM) pamoja na DAP-K na vyama vingine chipukizi.
Chaguzi hizi zinachukuliwa kama kipimo muhimu cha nguvu za kisiasa katika maeneo husika kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027, huku Rais William Ruto na wandani wake wakifuatilia kwa karibu matokeo yake.