Vijana wafurahia vitambulisho baada ya ada kuondolewa
VIJANA katika kaunti-ndogo ya Mavoko wamejitokeza kwa wingi kuomba vitambulisho vya kitaifa na kuonyesha nia yao ya kushiriki katika Uchaguzi Mkuu wa 2027 kama wapigakura wa mara ya kwanza.
Hatua hiyo imechochewa na agizo la serikali la kuondoa ada kwa waombaji wa mara ya kwanza pamoja na kusitisha malipo ya kubadilisha au kuomba upya vitambulisho vinapopotea.
Msamaha huo wa miezi sita ulianza Oktoba mwaka jana.
na unatarajiwa kukamilika Aprili, ambapo ada ya Sh300 kwa waombaji wapya na Sh1,000 ya waliopoteza vitambulisho ziliondolewa.
Katika mji wa Mavoko, Kaunti ya Machakos, vijana wengi hapo awali walikuwa wakikwepa usajili wakilalamikia urasimu na ucheleweshaji.
Msajili wa Watu katika eneo la Mavoko Jennifer Wanjiru, kwa ushirikiano na maafisa wa utawala wa eneo hilo, ameanzisha zoezi la usajili mashinani katika kambi za machifu akilenga kusajili angalau vijana 5,000 kabla ya muda wa msamaha kuisha.
Vijana wamesema kitambulisho kitawasaidia kupata ajira na pia kuwapa fursa ya kujiandikisha kama wapiga kura.