UDA kimeng’aa katika chaguzi ndogo, ODM kikikula huu
CHAMA cha Orange Democratic Movement (ODM) kinakabiliwa na wakati mgumu kisiasa baada ya matokeo ya chaguzi ndogo za Februari 26, 2026 kuashiria kuyumba katika ngome zake za jadi, huku mshirika wake katika serikali jumuishi United Democratic Alliance (UDA) kikizoa ushindi mkubwa.
UDA ilinyakua kiti cha ubunge cha Isiolo Kusini pamoja na viti vitatu vya udiwani- Evuvore na Muminji katika Mbeere Kaskazini na Kabras Magharibi eneobunge la Malava.
Lakini zaidi ya takwimu, matokeo hayo yameibua mjadala mpana kuhusu mwelekeo wa siasa za 2027 na mustakabali wa ODM hasa baada ya kuridhika na kura 30 pekee katika uchaguzi mdogo wa Kabras Magharibi.
Hii, wachanganuzi wanasema ni dalili kwamba inapoteza ngome yake ya Magharibi.
Katika eneo la Gusii, ambalo kwa muda mrefu limekuwa likitazamwa kama ngome ya ODM chini ya ushawishi wa aliyekuwa kinara wake Raila Odinga, dalili za kupungua kwa mvuto wa chama hicho zimeanza kuonekana. Badala yake, Jubilee Party chini ya Naibu Kiongozi wake Fred Matiang’i imeanza kuibuka kama kitovu kipya cha siasa za eneo hilo.
Mnamo Novemba 27, 2025, wagombea wanaoegemea upande wa Matiang’i walishinda chaguzi ndogo zote tatu katika wadi za Nyamaiya, Nyansiongo na Ekerenyo. Wachambuzi wanasema mwelekeo huo unafaa kutia viongozi wa ODM tumbojoto.
Mchanganuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki anasema matokeo hayo si ya kubeza. “Chaguzi ndogo huwa ni kipimo cha mitandao ya chini kwa chini. Ukipoteza ngome yako, ujumbe unaokwenda nje ni kwamba msingi wako unayumba,” asema.
Ushindi mkubwa zaidi wa UDA ulikuwa katika ubunge wa Isiolo Kusini, ambako Mohamed Tubi alipata kura 7,352 akimshinda mpinzani wake kwa tofauti kubwa. Ushindi huo uliimarisha uwepo wa UDA Kaskazini mwa Kenya na kuonyesha uimara wa mtandao wake wa mashinani.
Katika Mbeere Kaskazini, UDA ilitwaa viti vya Evurore na Muminji, ikiimarisha ushawishi wake katika Mlima Kenya Mashariki, eneo linalohusishwa na Naibu Rais Kithure Kindiki.
Hata hivyo, pigo lililoumiza zaidi ODM lilitokea Kabras Magharibi, Kaunti ya Kakamega eneo linalochukuliwa kama ngome ya jadi ya chama hicho. Mgombea wa UDA Elphas Shalakha alipata kura 3,317 huku mgombea wa ODM akipata kura 30 pekee, matokeo yaliyowashangaza wengi.
Dkt Gichuki anasema hali hiyo ni matunda ya mabadiliko ya siasa nchini ambayo vigogo wa ODM wanapuuza wakiendelea kugawanyika.
“Kuna dalili za kukata tamaa kwa wanachama wa ODM kutokana na mgawanyiko unaoendelea. Huku chama kikijadili nafasi za juu katika mazungumzo ya kitaifa, wapigakura wa mashinani wanataka uwepo na ajenda inayoonekana,” asema.
“Rais Ruto anatabasamu kuona akipata ushindi katika ngome yake ya Mlima Kenya bila usaidizi wa aliyekuwa naibu wake Rigathi Gachagua huku ODM ikiendelea kusambaratika hata katika ngome yake ya Nyanza,” asema na kutaka kujiuzulu kwa naibu gavana wa Homa Bay Oyugi Magwanga baada ya kutofautiana na Gavana Gladys Wanga ambaye ni mwenyekiti wa ODM.
Kulingana na wachanganuzi, ODM pia inakabiliwa na changamoto za ndani: migawanyiko, suitafahamu kuhusu mkakati wa 2027, na mpasuko kuhusu iwapo iendelee kushirikiana na UDA katika mpango wa serikali jumuishi au ibaki kama chama cha upinzani.
Mchanganuzi wa siasa David Kioko anaonya kuwa taswira ya chama inaweza kuathiriwa zaidi na mkanganyiko huo. “Siasa ni mtazamo. Ukionekana hauna mwelekeo thabiti, wapigakura huanza kuhepa,” asema.
Anasema kwa UDA, ushindi huo unatoa taswira ya uthabiti na nidhamu ya kisiasa. “Chama kinaonyesha uwezo wa kuhamasisha wapigakura, kuweka mikakati ya mapema na kugeuza chaguzi ndogo kuwa majukwaa ya kupima nguvu kabla ya 2027,” asema.
Ingawa chaguzi ndogo mara nyingi huathiriwa na masuala tofauti Dkt Kioko anasema mgawanyiko ndani ya ODM unakifanya kizame badala ya
Kulingana naye, ODM inajiweka katika hatari ya kudharauliwa wakati wa mazungumzo na UDA au chama kingine chochote kufuatia mizozo inayokikumba.