Hisia mseto Trump akimuua Ayatollah
MAUAJI ya Kiongozi wa Kidini wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei jana yalitikisa ulimwengu huku Rais wa Amerika Donald Trump akishutumiwa pamoja na Israel kwa kuingilia mataifa mengine kwa ‘kisingizio’ cha ugaidi.
Khamenei, 86 amekuwa madarakani kwa miaka 36. Amekuwa mwiba kwa Amerika na wakati kadhaa aliwahi kunukuliwa akisema Iran haiwezi kusitisha uundaji wa silaha hatari za nyuklia.
Runinga za Iran jana asubuhi zilitangaza kifo cha Khamenei na kusema alikuwa ameuawa katika uvamizi ulioongozwa na Amerika na Israel mnamo Jumamosi Februari .
Baadhi ya raia walimiminika jijini Tehran wakilia na kulaani Israel na Amerika huku wakisisitiza lazima serikali ilipize kisasi kuhusu mauaji ya kiongozi wao.
“Tulifikiria kwamba habari hizo zilikuwa za uongo lakini tukabaini asubuhi kuwa ni kweli,” akasema mwanamke mmoja akiomboleza kwa mauti ya Khamenei.
“Niko tayari kujitoa mhanga kwa dini ya Kiislamu na Imamu Khamenei. Utawala wa Wayahudi na Trump utalipia vikali kwa kumuua kiongozi wangu,” akaongeza.
Atousa Mirzade, mwalimu wa shule ya msingi jijini Shiraz alisema hawezi kufurahia nchi za kigeni kumuua kiongozi wa taifa lake.
“Siwezi kufurahia kwa sababu sijui kitakachofanyika katika taifa langu. Tuliona kile kilichofanyika Iraq ambako ghasia na umwagikaji wa damu ulishamiri, afadhali tubakie na Jamuhuri yetu ya Kiislamu,” akasema Mwanafunzi wa Chuo Kikuu, Hossein Dabakhsh, 21 jijini Mashhad.
Hata hivyo, wapo baadhi ya raia nchini Iran walionekana wakisherehekea jijini Tehran wakisema kiongozi huyo wa kidini alikuwa dikteta asiyeheshimu haki. Sherehe hizo zilikuwa katika miji ya Dehloran na Karaj viungani mwa Tehran.
Katika mji wa Galleh Dar Kusini mwa Iran, watu waliangusha sanamu ya mwanzilishi wa nchi hiyo Ayatollah Ruhollah Kamenei aliyeasisi Jamuhuri ya Kiislamu ya Iran mnamo 1979.
“Naota? Ama tuko dunia nyingine?” akasema mwanaume aliyeangusha sanamu hiyo. Video nyingine ilionyesha sherehe katika mji wa Lapuee ambapo Pooya Jafari, 15 aliyeuawa wakati wa maandamano dhidi ya serikali ya Iran, Januari.
Maelfu ya raia wa Iran waliuawa katika maandamano hayo yaliyokuwa makubwa nchini humo tangu 1979.
Akitangaza kuuawa kwa Khamenei, Rais Trump aliwataka raia wa Iran watumie nafasi hiyo kupindua serikali ili kuleta uongozi mpya.
Iran jana bado ilikuwa ikishambulia vituo vya kijeshi vya Amerika katika mataifa mbalimbali ukanda wa Mashariki ya Kati.
Nchi kadhaa ikiwemo Kenya zilikatiza safari za ndege kutokana na hofu za kiusalama huku nyingine zikitoa wito wa kusitishwa kwa uvamizi dhidi ya Iran.
Hapa nchini, Mwenyekiti wa Baraza la Waislamu, Hassan Ole Naado alishangaa kwa nini Baraza la Umoja wa Kimataifa (UN) limekaa kimya na kusema kuwa umoja huo unapendelea Amerika na mataifa makubwa.
“Hiki kiburi cha Amerika sasa kimevuka mipaka na inashangaza asasi kama UN bado zipo,” akasema Sheikh Naado.
“Trump sasa ni adui wa dunia na Amerika ndiyo inafanya ugaidi kuliko mataifa mengine. Kumuua Ayatollah kunastahili kuamsha ulimwengu ili watu wakatae udikteta wa Amerika,” akaongeza.
Naye Mwenyekiti wa Baraza la Maimamu na Wahuburi Waislamu Kaskazini mwa Bonde la Ufa, Sheikh Abubakar Bini alisema inasikitisha sana kuwa Amerika inaendeleza dhuluma dhidi ya mataifa mengine.
“Machafu yanaponyamaziwa basi dunia inaweza kumalizika hata kabla ya wakati wake, huwezi kumwaga damu na Allah akuache. Mbona madola makubwa hayazungumzi? Kwani Trump hashikiki wala hawezi kukusolewa? Hata madola madogo kama Kenya pia yazungumzie ukatili huu,” akasema Sheikh Bini.
Tayari vita hivyo, vimefanya balozi za nchi mbalimbali katika ukanda wa Mashariki ya Kati na duniani zitoe tahadhari kwa raia wake kukaa ange.
Jana, Amerika na Israel bado zilikuwa zikishambulia Iran huku vita hivyo vikitarajiwa kuwa pia na athari za kiuchumi kwa ulimwengu hasa iwapo Iran itazufunga mkondo wa baharini wa Hormuz.