Lugha, Fasihi na Elimu

Makosa katika kutunga sentensi zinazozingatia ‘nyakati’ na ‘hali’

Na HELLEN NJAGI March 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TUNAPOTUNGA sentensi katika lugha ya Kiswahili huwa tunazingatia kanuni kama vile: Maana ya maneno, viambishi sahihi vya upatanisho wa kisarufi, viambishi vinavyofaa vya nafsi na viambishi sahihi vya wakati.

Baadhi ya nyakati tunazofaa kuzingatia viambishi vyake tunapotunga sentensi ni wakati uliopo, wakati uliopita, wakati ujao, wakati timilifu na wakati wa mazoea.

Pia tunapotunga sentensi huwa tunazingatia nyakati na hali. Wanafunzi wengi wana uwezo wa kutunga sentensi sahihi katika nyakati mbalimbali.

Hata hivyo, baadhi ya wanafunzi hukumbwa na changamoto wanapotunga sentensi katika nyakati na hali.

Changamoto hii hasa hujitokeza katika kuandika sentensi katika wakati uliopita hali ya kuendelea na wakati ujao hali ya kuendelea.

Aghalabu utapata sentensi kama: *Wanafunzi walikuwa wanasoma mwalimu alipoingia darasani. *Wananchi walikuwa wanapanda miti mvua ilipoanza kunyesha. *Mama atakuwa anapika chajio tutakapowasili nyumbani.

Mifano hii ya sentensi si sahihi. Mwandishi ametumia kiambishi cha wakati –na- badala ya –ki- ili kuonyesha kuwa sentensi hizo ziko katika hali ya kuendelea.

Ili kuzisahihisha tunafaa kusema: Wanafunzi walikuwa wakisoma mwalimu alipoingia darasani.

Wananchi walikuwa wakipanda miti mvua ilipoanza kunyesha. Mama atakuwa akipika chajio tutakapowasili nyumbani.

Ili mwanafunzi akabili changamoto hii, anafaa afanye mazoezi ya kutambua kiambishi cha wakati uliopita hali ya kuendelea na kiambishi cha wakati ujao hali ya kuendelea katika sentensi mbalimbali.

Pia mwanafunzi afanye mazoezi ya kutunga sentensi sahihi akizingatia nyakati na hali.