Kimataifa

Trump: Iran lazima inishirikishe inapochagua kiongozi mpya

Na REUTERS March 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS wa Amerika, Donald Trump amesema kuwa ana haki ya kuungana na Iran kuamua kiongozi wake mpya baada ya kuuawa kwa Kiongozi wao wa kidini Ayatollah Ali Khamenei wikendi iliyopita.

Matamshi ya Trump yanajiri wakati ambapo Iran ikiendelea kushambulia ubalozi na kambi za kijeshi za Amerika kwenye ukanda wa Mashariki ya Kati.

Amerika na Israeli nazo pia ziliendeleza mashambulizi yao dhidi ya Iran huku vita hivyo vikionekana kuendelea kwa muda usiojulikana.

Jeshi la Israeli limesema mashambulizi yake ya hivi karibuni dhidi ya Iran “yameutikisa” uongozi wa kidini wa Jamhuri hiyo ya Kiislamu.

Msemaji wa jeshi la Israeli Effie Defrin amesema, “Lengo la operesheni hiyo ni kusababisha uharibifu mkubwa ndani ya serikali ya kigaidi ya Iran hadi iondoe kitisho kilichopo na tunaendelea kusababisha madhara kwa uongozi uliopo. Ni muhimu kwangu kusema kwamba tayari Iran imetikisika.

Ilitikiswa na shambulio la kwanza Jumamosi asubuhi, wakati kiongozi wao alipouawa. Na kila siku tunaendelea kuudhoofisha zaidi hadi tishio liondoke.”

Kwenye mahojiano na Shirika la Habrai la Reuters, Trump alisema kuwa hawezi kukubali uteuzi wa Mojtaba Khamenei kuwa kiongozi mpya wa Iran.
Mojtaba, mwana wa kiume wa Ayatollah Khamenei, ana msimamo na uhasama mkali na Amerika kama tu babake.

“Tunataka kushirikishwa katika mchakato wa kumchagua kiongozi mpya wa Iran ambaye atajenga upya taifa hilo na kuwapa raia wake matumaini,” akasema Trump.

“Tutachagua mtu huyo pamoja na Iran na lazima tushirikishwe kwa sababu tunatakia taifa hilo mema,” akaongeza.

Kiongozi huyo pia aliwashaajisha wapiganaji wa Kurdi walioko Iraq waendelee kupiga vita uongozi wa sasa wa Iran kwa kuvuka na kuingia ndani ya taifa hilo.

Kurdi ilikuwa mwiba kwa utawala wa Ayatollah Khamenei lakini mara nyingi ilikuwa ikilemewa na vyombo vya serikali.

Wapiganaji wa Kurdi waliunga maandamano ya raia wa Iran dhidi ya uongozi wa Ayatollah mapema mwaka huu ambapo mauaji mengi ya raia waliokuwa wakilalamikia maisha magumu yaliripotiwa.

“Nawaunga mkono Wakurdi. Ni vyema iwapo sasa watavuka mpaka na kuwaokoa raia wa Iran,” akasema Trump.

Kundi hilo sasa linashirikiana na Israeli na Amerika tangu Iran ivamiwe mnamo Jumamosi iliyopita.

Aidha Trump hakuweka bayana iwapo Amerika imetoa silaha za kutekeleza mashambulizi ya angani kwa raia hao.

Trump pia amedai kuwa uongozi wa Iran umekuwa ukijaribu kuwafikia ili vita hivyo ambavyo vimekuwa vikiendelea kwa wiki moja visitishwe.

Aliongeza kuwa sasa mikakati ni kuhakikisha kuwa wanapunguza shinikizo kuhusu mafuta ulimwenguni.

“Wanatupigia simu na kutuuliza kama tutaafikiana? Niliwaambia mmechelewa sana,” akasema Trump katika Ikulu ya White House baada ya kukutana na kikosi cha Inter Miami.

“Tumezamisha meli zao 24 ndani ya siku tatu na bado tunatuma droni na kuendelea kuwaangamiza. Wakati huu bado hakuna mwanya wa mazungumzo,” akaongeza.

Haya yanajiri huku Israeli ikisema kuwa vikosi vyake vimevilenga vituo kadhaa vinavyotumiwa na wanamgambo wa Hezbollah kusini mwa Beirut kupanga operesheni zao.

Shirika la habari la Lebanon NNA limeripoti kuwa shambulio la droni la Israeli lilipiga jumba moja katika eneo la Beddawi karibu na Tripoli, na kumuua afisa mwandamizi wa Hamas, Wassim Atallah al-Ali, pamoja na mke wake.

Kiongozi wa Hezbollah, Naim Qassem, ameapa kuendeleza mapambano dhidi ya Israeli, akisema kundi lake limefanya takriban mashambulizi 15 yaliyolenga maeneo ya Israeli.