Wanaharakati watatu wataka sheria ya kura ya urais ya asilimia 50 itumike kwa nyadhifa zote
WANAHARAKATI watatu wamewasilisha kesi katika Mahakama Kuu wakitaka mabadiliko makubwa yafanywe katika mfumo wa uchaguzi nchini Kenya, wakipendekeza kwamba wagombea wote wa nyadhifa za kisiasa walazimike kupata zaidi ya asilimia 50 ya kura zilizopigwa ili kutangazwa washindi.
Kesi hiyo imewasilishwa katika Mahakama Kuu ya Nakuru na wanaharakati Laban Omusundi, Basele Galgesa na Benson Olwande.
Wameishtaki Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) pamoja na Mwanasheria Mkuu, wakidai mfumo wa sasa wa uchaguzi una mapungufu yanayodhoofisha uhalali wa viongozi wanaochaguliwa.
Kwa sasa, uchaguzi nchini hutumia mfumo ambapo mshindi hutangazwa kwa kupata kura nyingi zaidi kuliko wagombea wengine, hata kama hajaungwa mkono na zaidi ya nusu ya wapiga kura.
Mfumo tofauti hutumika katika uchaguzi wa rais, ambapo mgombea lazima apate zaidi ya asilimia 50 ya kura zote pamoja na kura moja zaidi ili kutangazwa mshindi.
Wanaharakati hao wanataka kanuni hiyo itumike pia kwa uchaguzi wa magavana, maseneta, wabunge na wawakilishi wa wadi.
Wanasema iwapo hakuna mgombea atakayefikisha kiwango hicho, basi uchaguzi wa marudio kati ya wagombea wawili waliopata kura nyingi zaidi ufanywe.
Kwa mujibu wa waliowasilisha kesi hiyo, mfumo wa sasa unaruhusu viongozi kuchaguliwa kwa kura chache sana, jambo ambalo linaweza kumaanisha kuwa hawaungwi mkono na wapiga kura wengi.
Wanasema katika baadhi ya chaguzi nchini, viongozi hutangazwa washindi kwa kupata kati ya asilimia 22 hadi 34 pekee ya kura zilizopigwa.
Wanatoa mfano wa uchaguzi mdogo wa ubunge wa Mbeere North, ambapo Leo Wamuthende alitangazwa mshindi kwa kura 15,802 kati ya kura 34,134 zilizopigwa.
Hii ina maana kuwa hakufikisha hata asilimia 50 ya kura, huku zaidi ya wapiga kura 18,000 wakiunga mkono wagombea wengine.
Kwa maoni yao, hali kama hiyo inaonyesha kuwa mfumo wa sasa hauhakikishi uhalali wa kidemokrasia kwa viongozi wanaochaguliwa.
Wanasema mamlaka ya wananchi yanapaswa kuwakilishwa na viongozi wanaoungwa mkono wa wengi, si wachache.
Katika kesi hiyo, wanaharakati wanataka mahakama itoe uamuzi kwamba hakuna mtu anayepaswa kutangazwa mshindi wa kiti cha ugavana, useneta, ubunge au uwakilishi wa wadi bila kupata zaidi ya asilimia 50 ya kura zilizopigwa.
Aidha, wameomba mahakama itoe amri ya muda ya kusimamisha uchaguzi wowote unaohusisha nyadhifa hizo hadi kesi hiyo iamuliwe kikamilifu.
Wanaharakati hao wanaamini kuwa hatua hiyo itaimarisha demokrasia nchini kwa kuhakikisha viongozi wanaochaguliwa wanaungwa mkono na wapiga kura wengi.
Kesi hiyo imepangwa kutajwa Machi 23 katika Mahakama Kuu ya Nakuru, ambapo IEBC na Mwanasheria Mkuu watahitajika kujibu hoja zilizowasilishwa na wanaharakati hao watatu.