Habari

Shakahola: Sheria kuanzishwa kudhibiti mahubiri nchini

Na SAMWEL OWINO March 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WABUNGE na viongozi wa kidini wamefikia makubaliano yanayopendekeza kuanzishwa kwa baraza la kusimamia makanisa ili kuepuka mahubiri ya kupotosha.
Baraza lililopendekezwa, litaiga mfano wa taasisi kama Chama cha Wanasheria Kenya (LSK), litasimamia na kufuatilia maudhui ya mahubiri, maadili ya kidini, utawala wa taasisi, na mafunzo ya wahubiri.
Hatua hii ni jitihada za kudhibiti wanaojifanya wachungaji huku wakiwapotosha wafuasi.
Katika kikao kilichofanyika Alhamisi, wanachama wa Kamati ya Malalamishi ya Umma ya Bunge walisema wakati umefika wa kuanzisha chombo cha kudhibiti mafunzo ya viongozi wa kidini.
Jaribio la awali la serikali kudhibiti makanisa au kuweka sifa ambazo wachungaji wanahitaji kuwa nazo lilikabiliwa na upinzani kutoka kwa wahubiri, ambao wanachukulia kazi yao kama wito kutoka kwa Mungu.
Ombi la sasa, lililowasilishwa na Mchungaji Josiah Njiru, mwenyekiti wa Shirikisho la Vyuo vya Mafunzo ya Kikristo Kenya, linaitaka Bunge kuweka sheria ili kuwezesha wahubiri wa makanisa ya kipentekoste na Kiinjilisti kuanzisha shirika la kusimamia mafundisho.
Iwapo litaundwa na Bunge, baraza hilo litaidhinisha taasisi na mafundisho, kutambua uzoefu wa awali, na kudumisha uadilifu wa mafundisho miongoni mwa wahubiri.
Litafuatilia mafunzo na mahubiri ndani ya makanisa ya Kipentekoste na mengine nchini, kuweka viwango vya mtaala na kuidhinisha taasisi zinazotoa mafunzo hayo, na kiwango cha elimu. Pia litaweka uwajibikaji na uadilifu katika mafunzo ya kidini.
Wachungaji walioandamana na viongozi wengine 10 wa kidini, walisema ni wakati wa kuboresha mafunzo ya wachungaji ili kuleta utulivu katika makanisa.
Walisema ingawa Mamlaka ya Mafunzo ya Kiufundi (TVETA) inaorodhesha shule za Biblia kama taasisi zinazojikita kwenye ujuzi wa kiufundi, haiwezi kutathmini uhalisi wa mafundisho au uwajibikaji wa maadili.
“Tunataka baraza linaloongozwa na imani linalothibitisha ujuzi wa wachungaji, malezi ya kiroho, na maadili, masuala ambayo TVETA haikuainishwa kusimamia,” walisema.
Pia walisema, ingawa Tume ya Elimu ya Vyuo Vikuu (CUE) inapaswa kuidhinisha mipango ya taasisi zinazotoa shahada rasmi, baraza litazingatia mafunzo yasiyo rasmi kupitia ushauri, mafunzo ya utendaji, na malezi ya kiroho.
Baraza hilo pia litashughulikia wachungaji ambao wamekuwa wakihudumu kwa miaka mingi bila mafunzo rasmi na kuwaidhinisha chini ya mpango wa kutambua ujuzi.
Walisema wachungaji waliowakilisha wamekuwa wakipanga ndoa za kiroho, kutia moyo familia, kuwatembelea waliopoteza wapendwa, na kutatua migogoro bila cheti au malalamiko. Sasa wanataka huduma zao zithaminiwe, uzoefu wao utambuliwe, na wito wao uheshimiwe kisheria.
Mwenyekiti wa kamati, Eric Muchangi, alikiri kwamba kuna haja ya sheria kuongoza shughuli za taasisi za dini.
Wabunge wengine kama Janet Sitenei na Peter Kihungi walipendekeza mamlaka ya kusimamia wachungaji ili kuendeleza maadili na kufanya Kenya iwe nchi ya Kikristo.
Ombi hili limezua tena mjadala wa kudhibiti makanisa na viongozi wa dini au kuruhusu Roho Mtakatifu kuwaongoza wahubiri.
Mapendekezo haya yanajumuisha kuanzishwa kwa Tume ya Masuala ya Dini, sehemu ya mapendekezo ya jopo kazi lililobuniwa na rais baada ya mauaji ya Shakahola ambapo watu 400 waliuawa kwa kufuata maagizo hatari ya kiongozi wa kiroho. Baada ya uhuru mwaka 1963, makanisa ya Kiafrika yalijitokeza na kuanzisha vituo vya mafunzo, na kuendeleza elimu ya kuhubiri kote nchini.
Hii ilisababisha kuanzishwa kwa maelfu ya shule za Biblia kote nchini. Huku baadhi ya makanisa yakiwa na rasilimali za kutosha, mengine hufanya shughuli chini ya miti au kukodisha majengo na ukumbi ili kueneza neno la Mungu kwa wafuasi wao