Watu 10 wafariki Nairobi kutokana na mafuriko
WATU kumi wamethibitishwa kufariki jijini Nairobi kutokana na mafuriko yaliyokumba maeneo mbalimbali baada ya mvua kubwa kunyesha kwa saa kadhaa.
Kamanda wa Polisi wa Nairobi, George Seda alisema watu 8 kati ya waliopoteza maisha walisombwa na maji, huku baadhi yao wakifariki wakiwa ndani ya magari yao.
“Kuna watu waliokuwa ndani ya magari yao na wakasombwa na maji. Kwa sasa tumethibitisha vifo kumi lakini huenda idadi ikaongezeka kadri shughuli za uokoaji zinavyoendelea,” alisema Bw Seda.
Kamanda huyo pia alifichua kuwa angalau magari 71 yalisombwa na mafuriko katika maeneo tofauti jijini baada ya barabara kuu kufurika na kufanya usafiri kuwa mgumu.
Miongoni mwa maeneo yaliyoathirika ni Pipeline na Embakasi ambako sehemu za Barabara ya Kware zilifungwa kabisa.
Maeneo mengine yaliyoripotiwa kuathirika ni Mukuru Kwa Njenga, Reuben, Viwandani, Kibra, Mathare, Huruma, Baba Dogo.
Shughuli za uokoaji bado zinaendelea katika baadhi ya maeneo huku mamlaka zikiwataka wakazi kuwa waangalifu na kuepuka kuvuka mito au maeneo yaliyofurika.