Siri ya Afrika dhidi ya njaa na mabadiliko ya tabianchi
MBEGU ndiyo nguzo kuu zaidi barani Afrika katika mapambano dhidi ya njaa na usalama wa chakula.
Kulingana na Dkt Yacouba Diallo, Katibu Mkuu wa African Seed Trade Association (AFSTA), mageuzi kwenye kilimo barani hayawezi kupatikana bila mifumo imara na dhabiti ya mbegu bora.
AFSTA ilianzishwa mwaka 2000 kwa lengo la kukuza sekta binafsi ya mbegu Afrika, kuratibu sera na kanuni za mbegu, kuimarisha upatikanaji wa mbegu zenye ubora, ikiwa ni pamoja na kuendeleza bioteknolojia.
“Bila mbegu faafu na bora zinazostahimili mabadiliko ya tabianchi, itakuwa vigumu kuangazia kero ya njaa na usalama wa chakula Afrika,” Dkt Diallo anasema.
Kila mwaka mwezi Machi, AFSTA huandaa Kongamano la Mbegu barani Afrika, na mwaka 2026 litafanyika Afrika Kusini, Katibu Mkuu wa muungano huo akisema litaleta pamoja wadauhusika kutoka sekta za utafiti, udhibiti, biashara na wakulima, ajenda ikiwa ni kuangazia usalama wa chakula.
Kwa sasa, mabadiliko ya tabianchi yamekuwa tishio kubwa kwa wakulima Afrika, na ni suala linalopaswa kutathminiwa kwa kina na kuibuka na suluhu.
Kiangazi na ukame wa muda mrefu, mvua zisizotabirika, mafuriko, pamoja na kuongezeka kwa wadudu na magonjwa vyote vimepunguza uzalishaji.

Dkt Diallo anasema sekta ya mbegu ipo mstari wa mbele katika kukabiliana na changamoto hizi, ili kuendeleza aina ya mazao yanayostahimili ukame, joto kali na kukomaa mapema.
“Tafiti zinaonesha kuwa kati ya asilimia 40 hadi 50 ya ongezeko la mavuno hutokana na matumizi ya mbegu bora,” anaelezea.
Watafiti kutoka sekta ya umma na binafsi wanaendelea kubuni aina mpya za nafaka na mboga zenye uwezo kuvumilia misukosuko ya hali ya hewa.
“Mbinu za kisasa kama vile uboreshaji wa vinasaba na jeni zimeongeza kasi ya upatikanaji wa aina maalum za mbegu, ikiwemo ustahimilivu dhidi ya wadudu na magonjwa,” Dkt Diallo anafafanua.
Hata hivyo, mafanikio haya yanategemea uwezo wa mifumo ya mbegu kusambaza teknolojia na bunifu kutoka maabara hadi mashambani.
Mifumo imara ya mbegu inachangia moja kwa moja usalama wa chakula na lishe, Katibu Mkuu Diallo anasisitiza.
Wakulima wanapopanda mbegu bora, mavuno huongezeka na upatikanaji wa chakula kuimarika.
Aidha, mifumo ya uboreshaji mazao imeanza kujumuisha mazao yenye virutubisho, hivyo kusaidia kupunguza utapiamlo.
Bara la Afrika bado lina pengo kubwa la mavuno ikilinganishwa na maeneo mengine duniani, na kuziba pengo hilo Dkt Diallo kwenye mahojiano na Akilimali kwa njia ya kipekee alidokeza kwamba kunaanza na mbegu.
Biashara ya mbegu Afrika nayo ina mchango mkubwa kiuchumi.
“Uratibu wa kanuni na kuondoa vikwazo vya mipakani kutaruhusu mbegu kusafirishwa kwa urahisi kutoka nchi moja hadi nyingine, hatua itakayochochea uwekezaji, ajira na uhamishaji wa teknolojia,” akasema.

Mwelekeo huu unawiana na malengo ya African Union na utekelezaji wa African Continental Free Trade Area (AfCFTA).
Kwa jumla, mageuzi ya kilimo Afrika yanahitaji sera rafiki kwa ubunifu, ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi, na uwekezaji katika utafiti na usambazaji wa mbegu bora.
Bila mbegu zenye ubora na zinazostahimili mabadiliko ya tabianchi, ndoto ya kutokomeza njaa barani itabaki kuwa kitendawili na hekaya za abunuasi.
Mbegu ndiyo msingi wa uzalishaji, chanzo cha mapato kwa wakulima na nguzo ya uhakika wa chakula kwa vizazi vijavyo.
Ni kwa sababu hiyo, Machi 2026 AFSTA itaandaa Kongamano nchini Afrika Kusini ili kujadili masuala hayo.