Mikakati maalum kuboresha sekta ya kahawa
Soko la Kunadi Kahawa la Nairobi (NCE) limezindua mpango maalum wa miaka mitano wa 2026–2030 unaolenga kuongeza mapato ya wakulima, kuboresha ufanisi wa shughuli na kuimarisha uwazi katika biashara ya kahawa nchini.
Mikakati hiyo, kulingana na NCE inalenga kuona wakulima wa kahawa wananufaika na kupata donge nono.
Akizungumza wakati wa uzinduzi jijini Nairobi, Afisa Mkuu Mtendaji wa NCE, Lisper Ndung’u, alisema mpango huo umebuniwa kuifanya kahawa ya Kenya iwe na ushindani mkubwa katika soko la kimataifa huku ukihakikisha wakulima wanapata thamani halisi ya mazao yao.
NCE ndiyo husimamia mnada wa kahawa yote inayozalishwa nchini, ikitoa jukwaa la wazi ambapo wanunuzi na wauzaji hukutana kufanya biashara.
Lisper alisema mkakati huo mpya unakuja wakati ambapo kahawa imetambuliwa kama zao muhimu na lenye thamani katika mageuzi yanayoendelezwa na serikali.
“Kwa mfumo mpya wa udhibiti na kahawa kutambuliwa kama zao la kipaumbele, tunataka kuhakikisha wakulima wanapata soko linalowapa thamani kutokana na jitihada zao,” alisema.

Sehemu muhimu ya mpango huo ni kuimarisha ufuatiliaji wa kahawa, uwazi na upatikanaji wa taarifa za soko kwa wakati halisi.
Kupitia mifumo ya kidijitali, wakulima wataweza kupata taarifa za bei na mwenendo wa soko kwa haraka, jambo litakalowasaidia kufanya maamuzi bora kuhusu uzalishaji, uchakataji na uwekezaji kwenye mnyororo wa kahawa.
Mkakati huo, pia, unawiana na mageuzi mapana ya sekta ya kahawa ambayo serikali imekuwa ikitekeleza tangu 2023 chini ya Ajenda ya Mabadiliko ya Kiuchumi ya Bottom-Up (BETA).
Amos Mariba, Katibu wa Utawala katika Idara ya Ushirika kwenye Wizara ya Ushirika na Biashara Ndogo na za Kati, alisema kuimarishwa kwa Soko la Kahawa la Nairobi ni sehemu muhimu ya mageuzi ya serikali.
Alisema uzalishaji wa kahawa nchini, ambao umekuwa ukishuka hadi karibu tani 40,000 kwa mwaka katika miaka ya karibuni, unalengwa kuongezeka zaidi ya mara mbili katika muda miaka ijayo.
“Kwenye mikakati ya mageuzi, serikali inalenga kuvuka tani 100,000 ifikapo mwaka 2027 na hatimaye kufikia zaidi ya tani 200,000 katika miaka ijayo,” akasema Mariba kwenye mahojiano na Akilimali.
Mageuzi hayo tayari yameanza kunufaisha wakulima. Kabla ya mabadiliko hayo, bei ya kahawa ghafi ilikuwa ikichezea kati ya Sh20 na Sh40 kwa kilo katika baadhi ya maeneo.
“Leo hii wakulima wengi wanapata kati ya Sh120 na Sh150 kwa kilo kupitia vyama vya ushirika,” afisa huyo akasema.

Moja ya sababu kuu za mabadiliko hayo ni Mfumo wa Malipo ya Moja kwa Moja (DSS) unaohakikisha fedha za mauzo ya kahawa zinawekwa moja kwa moja katika akaunti za wakulima.
Serikali pia imeongeza ugavi maalum wa fedha za kahawa, ndio Coffee Cherry Advance Revolving Fund (CCARF), hadi zaidi ya Sh10 bilioni ili kuwapa wakulima mikopo nafuu.
Kenya inaendelea kujulikana duniani kwa kahawa yake ya Arabica yenye ubora wa juu, hasa kutoka maeneo ya kilimo ya jadi katika Ukanda wa Kati na Mashariki mwa Kenya.
Hata hivyo, mabadiliko ya tabianchi yanaendelea kuwa changamoto, huku mvua zisizotabirika na joto linaloongezeka vikidhoofisha uzalishaji wa kahawa.
Wadau wanasema uwekezaji katika aina za kahawa zinazostahimili hali ya hewa na ukumbatiaji teknolojia za kisasa za kilimo utakuwa muhimu katika kuongeza mazao.
Kwa upande wa masoko, karibu asilimia 95 ya kahawa yenye thamani ya Dola milioni 289 iliuzwa nje ya nchi mwaka jana, 2025.
Masoko mapya hasa barani Asia na Mashariki ya Kati – UAE yanaendelea kuonyesha hamu kubwa ya kahawa ya Kenya.