Kimataifa

Mahakama India yapinga pendekezo la kuwa na mapumziko ya hedhi

Na MASHIRIKA March 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu ya India imekataa ombi lililowasilishwa mahakamani lililotaka kuanzishwa kwa sera ya mapumziko ya hedhi miongoni mwa wanawake wanaofanya kazi na wanafunzi wa kike, huku majaji wakisema hatua hiyo inaweza kuwafanya waajiri kusita kuajiri wanawake.

Jopo la majaji wawili lililoongozwa na Jaji Mkuu Surya Kant lilisema kuwa kutunga sheria ya lazima ya likizo ya hedhi kunaweza kusababisha waajiri kuwabagua wanawake kazini.

Majaji hao walisema iwapo mswada huo utadihinishwa, “hakuna atakayekuwa tayari kuajiri wanawake.”
Kwa mujibu wa mahakama hiyo, kutoa likizo maalum kwa wanawake wakati wa hedhi kunaweza pia kuwafanya wanawake vijana wajione hawako sawa na wenzao wa kiume kazini, jambo ambalo majaji walisema linaweza kudhuru maendeleo yao ya kitaaluma.

Mahakama ilitoa kauli hiyo ikisikiliza ombi lililowasilishwa na wakili Shailendra Mani Tripathi, aliyetaka serikali kuanzisha sera ya kitaifa ya likizo ya hedhi.

Tripathi alipendekeza wanawake wanaofanya kazi wapewe siku mbili au tatu za mapumziko kila mwezi ili kukabiliana na maumivu na changamoto zinazotokana na hedhi.

Hata hivyo, majaji walikataa ombi hilo wakisema kuwa sera kama hiyo inaweza kudumisha dhana potovu za kijinsia na kuathiri nafasi za wanawake kupata ajira.

Walionya kuwa waajiri katika sekta ya kibinafsi wanaweza kusita kuwaajiri wanawake ikiwa sheria itawalazimisha kutoa likizo ya ziada.

Mahakama iliongeza kuwa serikali inaweza kuchunguza suala hilo na kuunda sera ya likizo ya hedhi baada ya kushauriana na wadau mbalimbali.

Uamuzi huo umechochea tena mjadala mkali nchini India kuhusu iwapo likizo ya hedhi ni hatua ya maendeleo kwa haki za wanawake au inachangia kuendeleza dhana kuwa wanawake ni dhaifu kazini.

Mtaalamu wa afya ya umma na wakili Sukriti Chauhan aliikosoa mahakama akisema kauli hiyo inaendeleza unyanyapaa unaohusishwa na hedhi.

Alisema India ina sheria zinazolinda heshima kazini, usawa wa kijinsia na mazingira salama ya kazi.

“Kunyima wanawake likizo ya hedhi kunawalazimisha kufanya kazi katika mazingira yasiyo na hadhi au salama wakati wanapokuwa na maumivu,” alisema.

Hata hivyo, baadhi ya watu wanasema likizo maalum kwa wanawake inaweza kuwa ubaguzi dhidi ya wanaume, hasa katika jamii ambako hedhi bado ni mada ya aibu.

Katika maeneo mengine ya India, wanawake wanaopata hedhi bado huzuiwa kuingia mahekalu au kushiriki shughuli fulani za kijamii.

Licha ya mjadala huo, baadhi ya majimbo na kampuni tayari zimeanzisha sera za likizo ya hedhi.

Majimbo ya Bihar na Odisha huwapa wafanyakazi wanawake wa serikali siku mbili za likizo kwa mwezi, huku Kerala ikitoa likizo hiyo kwa wanafunzi wa vyuo na taasisi za mafunzo.

Pia, mwaka jana jimbo la Karnataka lilipitisha sheria inayowaruhusu wanawake kupata siku moja ya mapumziko kila mwezi wakati wa hedhi.

Kadhalika, baadhi ya kampuni kubwa zimeanzisha sera kama hizo kwa wafanyakazi wao wa kike.