Siasa

Ruto aingilia kati zogo la Joho, vigogo wa UDA Pwani kuhusu azma ya unaibu rais

Na WINNIE ATIENO March 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto ameingilia kati mvutano wa kisiasa unaotokota kati ya Waziri wa Madini, Uchumi wa Bahari na Masuala ya Ubaharia, Bw Hassan Joho na baadhi ya wanachama wa United Democratic Alliance (UDA) katika eneo la Pwani.

Rais alitoa wito uhasama huo usitishwe mara moja, akisema unatishia umoja wa kisiasa unaokuzwa kati ya chama chake na ODM.

Bw Joho amekuwa akikumbana na upinzani katika jitihada zake za kujiongezea ushawishi wa kisiasa katika eneo hilo, huku akionyesha nia ya kutaka kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto katika Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Azma yake haijapokelewa vyema na baadhi ya wanachama wa UDA ambao wanamwona Waziri wa Michezo na Masuala ya Vijana, Bw Salim Mvurya, kama mwakilishi wao halisi katika serikali ya kitaifa, huku pia wakimuunga mkono Naibu Rais Kithure Kindiki kuendelea kuhudumu katika wadhifa wake.

“Viongozi wa ODM na UDA, jukumu lenu la kufanya kazi kwa maelewano ni muhimu sana. Msiruhusu migogoro ya ndani kudhoofisha maendeleo yetu,” alisema Ijumaa, wakati wa kufuturu na waumini wa Kiislamu katika Ikulu ya Mombasa.

Alisisitiza kuwa, viongozi wa Serikali Jumuishi (broad-based) wanafaa kuwa kielelezo cha umoja wa kitaifa badala ya kuwa chanzo cha mgawanyiko. Rais Ruto aliwataka pia viongozi wa Pwani kuzungumza kwa sauti moja.

Migawanyiko

“Mmesikia kuna ‘fire’ na ‘power’ katika serikali hii jumuishi. Mkiviunganisha viwili hivyo, tutapata nguvu kubwa itakayolisukuma taifa hili kufikia viwango vipya,” alisema, akirejelea kauli mbiu maarufu za naibu wake na kiongozi wa ODM Oburu Oginga mtawalia.

“Ninawasihi msigawanye nchi yetu. Umoja wa taifa letu uko mikononi mwenu,” aliongeza rais.

Bw Mvurya, akizungumza kwa uwazi usio wa kawaida, alisema anashangaa kuona nafasi ya naibu rais imegeuzwa kuwa mjadala wa umma.

Alisema naibu rais hachaguliwi na makundi ya kikanda bali huteuliwa na mgombea urais pekee.

“Tumeshtushwa sana kuona suala la nafasi ya naibu rais wa 2027 limegeuzwa kuwa mjadala mkubwa. Hili linaturudisha nyuma,” alisema Bw Mvurya.

“Nataka kuwaambia: hiyo ni haki ya mgombea urais. Ndani ya UDA, ni Rais Ruto aliye na mamlaka hayo. Tuache kuwapa watu wa Pwani matumaini kwa jambo ambalo halipo,” aliongeza.

Bw Mvurya pia alimtetea Prof Kindiki akimtaja kuwa msomi mwenye hadhi ya juu na rekodi bora ya kimataifa.

Alionya kuwa, shinikizo kwa rais kubadili tiketi ya uchaguzi wa 2027 linaweza kusababisha eneo la Pwani kujitenga kisiasa.

Wakati wa futari hiyo, Spika wa Seneti, Bw Amason Kingi, alimwahidi Rais Ruto kwamba atafanya kazi pamoja na Bw Mvurya kuimarisha uungwaji mkono wa Pwani katika uchaguzi mkuu ujao.

Bw Joho hakuhudhuria hafla hiyo, akituma ujumbe kupitia kwa Gavana wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir, kwamba alikuwa ameenda kufanya Umrah.

Hija hiyo ni ya hiari ya Kiislamu inayofanywa katika mji mtakatifu wa Mecca nchini Saudi Arabia ambayo Waislamu wanaweza kuifanya wakati wowote wa mwaka.