Gachagua amjibu Ruto, aibua madai mapya ya ufisadi
ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua amemjibu vikali Rais William Ruto, akimlaumu kwa “kudunisha hadhi ya urais” kwa kuzungumzia maisha ya kibinafsi ya watu badala ya masuala mazito yanayoikabili nchi.
Akizungumza katika makao makuu ya chama chake alipokuwa akimpokea aliyekuwa Seneta Maalum Millicent Omanga, Gachagua alisema Rais anapaswa kuangazia masuala muhimu ya kitaifa badala ya kushambulia watu binafsi.
“Huna haja ya kuzungumzia maisha ya mtu binafsi au kama ana mke au la. Unapaswa kuangazia masuala mazito kama miundombinu, usalama wa nchi na hali mbaya ya huduma za afya. Hayo ndiyo Wakenya wanataka kusikia kutoka kwa Mkuu wa Nchi,” alisema.
Kauli zake zilikuwa majibu ya hotuba za hivi karibuni za Rais Ruto ambapo amekuwa akiwawakia wakosoaji wake wakati mwingine akigusia maadili, mwonekano wa kimwili na maisha ya faragha ya baadhi ya viongozi.
Gachagua pia aliibua madai mapya ya ufisadi kuhusu mradi wa mabilioni ya fedha wa Railway City jijini Nairobi.
Alidai kuwa kampuni ya China Civil Engineering Construction Corporation (CCECC), iliyotoa zabuni ya chini zaidi, haikupewa kandarasi kwa sababu haikutoa hongo ya Sh7 bilioni.
Badala yake, alisema kandarasi hiyo ilipewa China Road and Bridge Corporation (CRBC) kwa gharama ya Sh30 bilioni, hatua aliyodai iliongeza gharama ya mradi huo kwa mabilioni ya pesa za walipa kodi.
“Tungependa kuarifu Ubalozi wa Uingereza jijini Nairobi kwamba wanapaswa kufuta mradi huo na zabuni ya ujenzi wa Railway City,” alisema.
Gachagua pia alidai kuwa kampuni nyingine za China zimekuwa zikinyimwa kandarasi kwa kukataa kutoa malipo yasiyo halali.
“Kampuni zote za China zimekataliwa na hazipewi kandarasi. Rais aliamuru CRBC iwe kampuni pekee inayopata kandarasi. Imekuwa njia ya kupitisha na kufyonza mabilioni ya fedha za walipa kodi,” alisema.
Katika mashambulizi yake ya kisiasa, Gachagua alimkosoa Rais kwa kauli zake za hivi karibuni kuhusu viongozi wengine, akisema mazungumzo ya kitaifa yamegeuzwa kuwa ya mzaha.
“Sisi hatuna shida na masikio yako, tunataka yawe makubwa zaidi ili uweze kusikiliza wananchi,” alisema kwa kejeli.
Aliongeza kuwa nchi inakabiliwa na changamoto kubwa kama deni la taifa, sekta ya afya inayoyumba na miundombinu duni, masuala ambayo alisema yanahitaji kipaumbele.