Ruto ahimiza Wakenya kudumisha umoja na upendo Waislamu wanaposherehekea Idd
RAIS William Ruto amewataka Wakenya kudumisha umoja na upendo wakati huu ambapo waumini wa Kiislamu wanaadhimisha siku kuu ya Idd ul-Fitr.
Kwenye taarifa aliyoitoa Machi 20, 2026 baada ya kukamilika kwa Mwezi Mtukufu wa Ramadan kiongozi wa taifa aliwataka Wakenya kuonyesha ukarimu na upendo wakati wa msimu huu.
Dkt Ruto alikariri umuhimu wa siku kuu ya Idd ul-Fitri katika kujenga imani ya waumini wa Kiislamu huku ikiwawezesha kuendeleza mshikamano na Wakenya wa dini nyingine “ili kufikinisha uwiano wa kitaifa.”
“Tunaungana na jamii ya Kiislamu kusherehekea Idd Ul-Fitri kufuatia kukamilika kwa mwenyezi mtukufu wa Ramadan, msimu wa kujitolea, kujenga imani, kuomba, kuwasaidia wasiojiweza katika jamii na kutafakari kuhusu thamani ya maisha. Naomba kwamba roho ya imani na ibada iendelee kutuongoza na taifa letu,” akaeleza kiongozi wa taifa.
“Idd ni siku muhimu ya kusherehekea maadili kwa imani, umoja na kwa kutoa shukrani. Tunaposherehekea hebu tuwakumbuke wanyonge na wasiojiweza katika jamii kwa kuwaonyesha ukarimu ili wote wafaidi kutokana na baraka hizi,” Dkt Ruto akaongeza.
Rais alieleze matumaini kuwa sherehe za Eid-ul Fitri zitapalilia amani, kujenga mshikamano wa kijamii na kuibua matumaini miongoni mwa raia kote nchini.