Aliyekuwa mfungwa Mwendwa, 35 hatimaye ajiunga na chuo kikuu
MFUNGWA wa zamani ambaye juma lililopita aliwashangaza wengi alipomtafuta hakimu aliyemhukumu kifungo cha miaka minne gerezani ili kumshukuru sasa amejiunga na chuo kikuu.
Mwendwa Kilatya Nthenge,35, Ijumaa alijiunga na chuo kikuu cha Africa Nazarene kilichoko eneo la Ongata-Rongai, kaunti ya Kajiado.
Jaji aliyemhukumu, Bw Eugene Pascal Nabwana ndiye aliyemsafirisha kwa gari lake la kibinafsi kutoka eneo la Syokimau, kaunti ya Machakos hadi Africa Nazarene University kujiunga rasmi na chuo hicho.
Bw Nabwana pia alikuwa wa kwanza kumsaidia kwa kumlipia sehemu ya karo yake ya muhula wa kwanza chuoni anakosomea cheti cha masuala ya Biashara na Usimamizi.
Akizungumza na Taifa Leo, Bw Nabwana alimtaja Bw Kilatya kuwa mtu aliyebadilika na kwamba furaha yake ni kumuona ametimiza ndoto yake ya masomo, kupata kazi nzuri na kujiendeleza maishani.
“Kwanza kabisa nashukuru shirika la habari la Nation Media Group kwa kuangazia taarifa ya Kilatya. Nimeonelea vyema nimfikishe hapa angalau asajiliwe rasmi chuoni. Nimelipa sehemu ya karo ila deni bado ni kubwa. Ningeomba sana wahisani zaidi wajitokeze ili kuchangia Bw Kilatya asome chuoni bila kutatizwa,” akasema Bw Nabwana.
Taifa Leo pia iliona barua ya usajili ya Bw Kilatya ya chuo cha Africa Nazarene ambapo nambari yake ya usajili ni CBM2027/083.
Ili kufanikisha masomo yake, nambari maalum ya kumchangishia karo ilitolewa kama Paybill Number 7291071 ilhali akaunti yake ikiwa ni CBM2027/083.
Katika mahojiano na Taifa Leo, Bw Kilatya hakuficha furaha yake kujiunga na chuo cha Africa Nazarene ambacho kimekuwa ndoto yake ya muda mrefu.
“Nimefurahi. Nashukuru Nation Media Group. Zaidi ninamshukuru jaji Nabwana. Amedhihirisha moyo wa upendo. Yeye ni zaidi ya mzazi wangu sasa. Mungu ambariki kwa msaada wake,” akasema Bw Kilatya.
Aliahidi kutia bidii masomoni.
“Nitasoma kwa bidii na punde nikikamilisha na kuhitimu cheti, nitajikaza nifanye Diploma kabla ya kusomea Digrii. Wote waliochangia na watakaochangia kufaulu kwangu wabarikiwe,” akasema Bw Kilatya.
Naibu Chansela anayehusika na masuala ya wanafunzi na masomo katika chuo kikuu cha Africa Nazarene, Prof Simon Obwatho, alimtaja Bw Kilatya kuwa mtu aliyebadilika kikweli kutoka kwa ‘mui hadi kuwa mwema.”
Prof Obwatho pia alimshukuru Bw Kilatya kwa kuchagua taasisi ya Africa Nazarene alikosajiliwa kuanza muhula wake wa 2026.
“Tutashirikiana naye kwa karibu. Twataka awe kielelezo cha wengine ambao wanapitia changamoto kama zake kwamba bado unaweza kufungwa jela lakini ukabadilika, kuwakielelezo na kioo cha jamii,” akasema Bw Obwatho.
Julai 2,2026, Bw Kilatya alimtembelea Bw Nabwana ofisini mwake katika jumba la mahakama ya Wamunyu, kaunti ya Machakos wiki kmfafanulia kuwa baada ya kumfunga miaka minne gerezani kwa kosa la wizi wa mifugo, alitumia muda huo kusoma, kujisajili katika mtihani wa kidato cha nne (KCSE) alioufanya 2025.
Alipata alama ya D.
Punde alipokamilisha kifungo cha mwaka huu, alionelea amtafute Bw Nabwana kumshukuru na pia kumuomba kabisa msaada wa kuendeleza masomo yake.
“Nilitii ushauri wako. Nikasoma kwa bidii nikiwa jela na kupata alama ya D nikiwa gerezani. Bado nina hamu kubwa ya kuendeleza masomo yangu ila sina namna.Nisaidie nipate ufadhili nisome,” akasema Bw Kilatya.
Hivyo Ijumaa Bw Kilatya alionekana kuwa mwingi wa furaha alipokubaliwa na kusajiliwa chuoni Africa Nazarene kuanza rasmi masomo yake ya juu.