Nyota wa filamu Chuck Norris amefariki dunia
MUIGIZAJI mashuhuri wa filamu za mapigano na bingwa wa zamani wa karate, Chuck Norris, amefariki dunia, familia yake ilitangaza kupitia taarifa iliyochapishwa katika akaunti yake ya Instagram Ijumaa Machi 20, 2026.
Katika taarifa hiyo, familia yake ilisema Norris aliaga dunia Alhamisi akiwa karibu na wapendwa wake.
“Ingawa tungependa faragha kuhusu kilichotokea, tafadhali fahamuni kuwa alikuwa pamoja na familia yake na alikuwa na amani,” ilisema taarifa hiyo.
Norris, ambaye aliwahi kuwa bingwa wa dunia wa uzani wa kati wa karate bila kushindwa mara sita, alipata umaarufu mkubwa katika miaka ya 1980 kupitia filamu za mapigano.
Alijulikana kwa kuigiza mashujaa waliokuwa wapiganaji jasiri, askari au maafisa wa sheria waliokabiliana na wahalifu na magaidi.
Baadhi ya filamu zilizompa umaarufu mkubwa ni pamoja na Code of Silence, Missing in Action na The Delta Force.
Aidha, alijulikana sana kupitia kipindi maarufu cha televisheni Walker, Texas Ranger, ambacho kilimwonyesha kama afisa wa sheria anayepambana na wahalifu kwa ustadi wa hali ya juu wa karate.
Kwa mujibu wa jarida la burudani la Amerika, Norris alikuwa amelazwa hospitalini Hawaii Alhamisi kabla ya kifo chake.