Habari za Kaunti

Wakazi wapata afueni Bomba la maji likikarabatiwa

Na STANLEY NGOTHO March 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Ulimwengu unavyoadhimisha Siku ya Maji Dunian, makumi ya wanawake katika maeneo ya ukame ya Kaunti ndogo ya Kajiado West walipata afueni baada ya ukarabati wa bomba kubwa la maji ambalo lilikuwa limeharibika na kutotumika kwa miaka 15.

Kwa zaidi ya muongo mmoja, kuharibika kwa bomba la maji la kilomita 78 la Sampu lililojengwa miaka ya 1950, ambalo hapo awali lilikuwa likipeleka maji safi kutoka vyanzo vya maji vya Nkurumani hadi mji wa Magadi, kuliwalazimu wanawake kutembea karibu kilomita 20 kila siku kutafuta maji.

Katika kipindi hicho cha miaka 15 ambapo bomba hilo lilikuwa halifanyi kazi, wakazi walilazimika kutegemea mabwawa madogo yasiyo salama na maji ya mvua , hali iliyoweka familia katika hatari ya kiafya na usalama.

Eneo la Magadi limekuwa likikumbwa na uhaba wa maji kwa muda mrefu kutokana na ukosefu wa mvua ya kutosha unaosababisha ukame wa mara kwa mara. Hivi sasa, wakati sehemu nyingi za nchi zinaposhuhudia mafuriko, baadhi ya maeneo ya Magadi bado yanapokea mvua chache sana.

“Kwa miaka mingi wanawake wamekuwa wakivuka maeneo magumu wakitafuta maji, wakitumia punda kubeba maji hadi nyumbani. Wanawake wengi hutumia muda mwingi mchana kutafuta maji ambayo yamekuwa bidhaa adimu,” alisema Evalyn Silau.

Hata hivyo, sasa matumaini yameanza kurejea baada ya kampuni ya Tata Chemicals kukarabati bomba hilo, mradi uliowachukua wahandisi karibu miaka miwili kukamilisha. Mradi huo ulizinduliwa Jumamosi, siku moja kabla ya maadhimisho ya Siku ya Maji Duniani.

Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, Swaminathan Nagarajan, aliwahimiza wakazi kulinda miundombinu hiyo dhidi ya uunganishaji haramu wa maji na uharibifu ili kuhakikisha upatikanaji wa maji safi unaendelea kwa uhakika.

Alisema uzinduzi wa mradi huo mkubwa unaangazia kaulimbiu ya mwaka huu ya Siku ya Maji Duniani ambayo ni Maji na Usawa wa Kijinsia: Maji Yanapotiririka, Usawa Hukuzwa.

“Kwa miaka 15 familia na mifugo wamekuwa wakiteseka. Wanawake ndio wamebeba mzigo mkubwa wa uhaba wa maji. Huu we wito kwa jamii kulinda mradi huu dhidi ya uharibifu na uunganishaji haramu ili kuhakikisha kila kijiji kinapata maji kwa usawa,” alisema.

Mkurugenzi wa Bodi ya Soda Ash, Dkt Stephen Moiko, alisema ukarabati huo ulikuwa umechelewa sana ikizingatia uhaba sugu wa maji katika eneo hilo.

Kando na bomba hilo lililokarabatiwa, matangi makubwa ya maji, maeneo ya kunyweshea mifugo na miundombinu ya usafi kwa wafugaji zimewekwa kimkakati kusaidia familia na mifugo

Wanawake katika vijiji vilivyoathiriwa wamepokea mradi huo kwa furaha wakisema umeondoa mzigo mkubwa wa kutembea umbali mrefu kutafuta maji, jukumu ambalo kwa miaka mingi lilikuwa likiwakabili wao zaidi

“Sasa tutatumia muda wetu kufanya shughuli bora zitakazoboresha maisha yetu, hasa kiuchumi, badala ya kutumia muda mwingi kutafuta maji,” alisema Janet Mokpo.

Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana, Jackson Ole Sapiti, aliyeongoza uzinduzi huo, alihimiza jamii ya wafugaji kutumia fursa ya upatikanaji bora wa maji kuboresha maisha yao.

Kanisa la Anglikana pia lilichangia pakubwa katika ujenzi wa bomba la awali la maji.

Kwa wakazi wa Magadi, Siku ya Maji Duniani si tu siku ya kuongeza uelewa — bali ni ishara ya kurejea kwa chanzo cha uhakika cha maji baada ya miaka mingi ya mateso.