Maswali huku Tuju akitoweka zogo la mali yake likizidi
WAZIRI wa zamani na ambaye pia alihudumu kama Katibu Mkuu wa Chama cha Jubilee anayekabiliwa na kipindi kigumu kuhusu mali yake, Raphael Tuju jana iliripotiwa kutoweka.
Wakili wake Paul Nyamodi alithibitisha kuwa Bw Tuju na dereva wake Steve Mwanga, walitoweka Jumamosi jioni.
Kwa mujibu wa Bw Nyamodi, mwanawe Tuju alipokea simu kutoka kwa Kamanda wa Kituo cha Polisi Karen (OCS) aliyemfahamisha kuwa gari la baba yake lilikuwa limeonekana kwenye barabara ya Miotoni Lane lilikoachwa Jumamosi usiku.
“Tunataka kukufahamisha tu kuwa Raphael Tuju alikuwa na shughuli katika kituo cha redio cha Ramogi jana (Jumamosi) jioni saa moja. Lakini hakufika kwa shughuli hiyo,” Bw Nyamodi alisema jana jioni.
Alisema ripoti kuhusu mtu aliyetoweka imeandikishwa katika Kituo cha Polisi cha Karen.
Matukio haya yamejiri siku chache baada ya maafisa wa polisi kutwaa kimabavu mali yake iliyopo Karen kwenye oparesheni isiyo ya kawaida usiku wa manane.
Bw Tuju wiki mbili zilizopita alidai kuwa kikosi kikubwa cha polisi kilivamia makazi yake ya Dari Park, mtaani Karen, mwendo wa saa tisa usiku, wakawafurusha walinzi na kufunga majengo hayo bila kibali cha korti.
“Waliwarusha nje walinzi wangu. Wametwaa kituo changu kimabavu,” alisema Bw Tuju siku chache kabla ya kutoweka.
Kulingana naye, oparesheni hiyo ilitatiza biashara zisizopungua 25 zinazoendesha shughuli makazini humo, ikiwemo afisi yake.
Bw Tuju vilevile alidai kuwa watu wenye ushawishi mkubwa wanahusika na jaribio la kutwaa mali yake, akidai hapo awali kwamba alikataa ombi la mwanasiasa mashuhuri.
Ripoti kuhusu kutoweka sasa zimezidisha maswali kuhusu makabiliano ya muda mrefu ya kisheria kati ya Bw Tuju na Benki ya East African Development kuhusu mkopo wa Sh2.2 bilioni.
Rais William Ruto na Kinara wa ODM Dkt Oburu Oginga, imeripotiwa wamesema masaibu ya waziri huyo wa zamani yanaweza kutatuliwa tu akifuata sheria.
Hii ni baada ya kubainika kwamba mali ya Bw Tuju ilinunuliwa kupitia mnada na suluhu pekee ni kumrejeshea hela alizonunulia mali hiyo.