Matumaini ya Arsenal kushinda ‘quadruple’ yayeyuka baada ya kipigo cha Man City
MATUMAINI ya miamba wa soka Arsenal kushinda mataji manne msimu huu yaliyeyushwa kwa njia aina yake pale Manchester City ilipowatandika 2-0 kwenye fainali ya Carabao Cup, ugani Wembley.
Vinara wa Ligi Kuu ya Uingereza Arsenal walifungwa mabao hayo katika kipindi cha pili wakati nyota wa Man City Nico O’Reilly alipozidia maarifa safu ya ulinzi dakika ya 60 na 64, kwenye fainali hiyo iliyosakatwa Jumapili, Machi 22, 2026.
Vijana wa Mikel Arteta wamekuwa wakifukuzia mataji manne msimu huu wa 2025-26: wakiwa kileleni mwa EPL kwa alama 9, wakifuzu kwa robo fainali ya Klabu Bingwa barani Ulaya, wakiwa raundi ya tano ya FA Cup, na vilevile kwenye fainali ya League Cup, almaarufu ‘Carabao Cup’ ambayo wameishia kupoteza.
Katika mechi hiyo ya fainali, The Gunners walianza mchezo kwa mashambulizi makali yakiongozwa na nyota Viktor Gyokeres akishirikiana na kiungo Kai Havertz, ingawa hawakufaulu kuona lango la Man City.
Hata hivyo, hali iligeuka muda mfupi baadaye wakati vijana wa kocha Pep Guardiola walipoanza kubana Arsenal kiasi cha kuwafungia kabisa kuunganisha pasi yoyote kwenda mbele.
Kwa kipindi kirefu katika dakika za mwishoni mwa kipindi cha kwanza, safu ya ulinzi ya Arsenal ilionekana kulemewa kabisa, hali iliyoendelea vivyo hivyo katika kipindi cha pili huku golikipa Kepa Arrizabalaga akifanya masihara yaliyopelekea kufungwa kwa bao la kwanza katika dakika ya 60.
Mshambuliaji O’Reilly aliongeza la pili dakika nne baadaye kutokana na krosi iliyotokana na mashambulizi ya mfululizo na baada ya hapo ikamjuzu Arteta kufanya mabadiliko kwa matumaini ya kubadilisha mchezo.