Utata wa miili ya Nyamira kuzikwa Kericho
UTATA umezuka kuhusu miili 14 ambayo ilizikwa kisiri katika Kaunti ya Kericho huku wamiliki wa makaburi, maafisa wa utawala wa kieneo, polisi na serikali ya kaunti hiyo wakionekana kutokuwa na ufahamu wowote kuhusu tukio hilo.
Maswali yameibuka kuhusu jinsi miili hiyo ilivyosafirishwa kutoka Nyamira kwa amri ya korti bila asasi husika za serikali kujua, kisha ikazikwa Kericho.
Pia imebainika kuwa vijana watatu ambao walikodishwa kuondoa miili hiyo na kuizika walilipwa Sh1,000 kila mmoja.
“Tulilipwa Sh1,000 kuchimba kaburi na Sh1,000 nyingine kuondoa miili kwenye gari na kuizika.
“Hatukuwa na majukumu mengine,” mmoja wa vijana hao akaambia Taifa Leo akisema walionywa dhidi ya kuzungumza na wanahabari.
“Hatuwajui waliotukodisha kwa sababu walikuwa wamevaa barakoa. Hata hivyo, si mara ya kwanza tunafanya kazi hii kwa sababu ndiyo njia tunayojizumbulia riziki,” akaongeza.
Ripoti zinaarifu kuwa zaidi ya miili 60 kutoka Nyamira huenda ilizikwa kisiri kwenye makaburi hayo bila kujulikana ni asasi gani husika iliyofanya hivyo.
Baraza la Kitaifa la Makanisa nchini (NCCK) ambalo linamiliki makaburi hayo mjini Kericho pia lilisema hakuna aliyeomba idhini kutoka kwao kabla ya kuizika miili hiyo.
Fredrick Odhiambo ambaye ni Mkuu wa Mipango ya Dharura ya Kupambana na Majanga Vocal Afrika, alidai kuwa karibu miili 70 huenda imezikwa katika makaburi ya Kericho miezi ya juzi.
“Uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa mbali na miili hiyo 14 iliyozikwa mnamo Alhamisi, mingine tisa ilizikwa mwezi uliopita na 42 ililetwa na lori mwaka jana. Hili suala linahitaji uchunguzi wa ndani kabisa,” akasema Bw Odhiambo.
“Shirika la Ujasusi nchini (NIS) na Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wanastahili kuwapa Wakenya ufafanuzi kuhusu suala hili. Uchunguzi wa ndani lazima ufanyike,” akasema Bw Odhiambo.
Ufichuzi huo umeibua maswali kuhusu mauaji ya kiholela ambapo watu wamekuwa wakitoweka kisha kupatikana wakiwa wafu kwenye mochari.
“Kama si waathiriwa wa mauaji ya kikatili na kiholela, mbona walizikwa haraka tena kisiri?
“Mbona asasi husika katika Kaunti ya Kericho hazikufahamishwa?” akauliza.
Jana Afisa wa DCI anayehusika na uchunguzi wa visa vya mauaji Martin Chaguto alichukua usukani na sasa makaburi hayo yamezingirwa huku yakilindwa na maafisa wa polisi.
Bado amri ya mahakama inasubiriwa ili miili hiyo ifukuliwe.
Gavana wa Kericho, Eric Mutai alithibitisha kuwa serikali yake haikuwa na maafikiano na kaunti jirani kuhusu kuzikwa kwa miili hiyo katika gatuzi lake hilo.
“Kericho si makaburi kwa kaunti nyingine wala hatukuwa na makubaliano kuhusu suala hilo.
“Hata sisi tumeshtuka,” akasema Dkt Mutai akitaka miili yote ifukuliwe mchana kisha ihifadhiwe katika Hospitali ya Rufaa ya Kericho huku uchunguzi wa kina ukiendelea.
Jana, maafisa wa afya katika Kaunti ya Nyamira walithibitisha kuwa miili 13 ambayo jamaa zao hawajajitokeza, ilisafirishwa hadi Kericho kuzikwa lakini haijabainika iwapo ni kati ya 14 ambayo ilipatikana makaburini Kericho.