Habari

Msitumie vifo vya binti zetu kujikweza kisiasa, familia zaonya

Na MWANGI MUIRURI, MERCY MWENDE March 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

FAMILIA mbili katika kaunti za Nyeri na Murang’a zimewataka wanasiasa kuacha kutumia majina ya wapendwa wao waliofariki katika mijadala ya kisiasa iliyoenea katika mikutano ya hadhara wiki mbili zilizopita.

Familia za Regina Wairimu na Maureen Kinyua zilisema kauli za kisiasa kuhusu vifo vya wapendwa wao zimekuwa zikifufua maumivu na huzuni ambazo wamekuwa wakijaribu kusahau kwa muda mrefu.

Katika Kaunti ya Murang’a, familia ya Regina—aliyekuwa mwanafunzi wa mwaka wa nne wa uhandisi katika Chuo Kikuu cha Dedan Kimathi, imetaka idara za usalama na wanasiasa kuacha kuwashinikiza kufungua upya uchunguzi wa kifo chake.

Akizungumza mjini Kenol, msemaji wa familia, Francisca Wambui, alisema wamekuwa wakipokea simu na ziara kutoka kwa watu wanaodai kuwa maafisa wa serikali wakitaka uchunguzi mpya.

“Wengine wameahidi familia pesa hadi Sh10 milioni ili kuitisha mkutano wa wanahabari na kumtaja mshukiwa,” alisema.