Makala

Wito serikali iimarishe sera ya kutetea haki za wajane nchini

Na WINNIE ONYANDO March 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BAADA ya kifo cha mumewe mwaka wa 2008, maisha ya Josephine Wainaina yalibadilika ghafla.

Akiwa na umri wa miaka 53 sasa, anakumbuka kwa uchungu jinsi alivyohangaika pamoja na watoto wake wawili.

“Nilipoteza kila kitu. Tulitoka pale tulipokuwa tunaishi na kuanza maisha upya,” anasema.

Alilazimika kuhangaika akitafuta kazi za vibarua ili kuwalisha watoto wake.

Kulingana naye, safari yake imejaa maumivu, kupoteza mali na kupambana kila siku kukidhi mahitaji yake na ya watoto wake hali ambayo wajane wengi nchini wanapitia kimya kimya.

Kulingana na Askofu EllyJoy Moi wa kanisa la Holy Well of Bethel, Limuru, wajane wengi wanakumbana na changamoto kadhaa ikiwemo kunyanyaswa, kunyimwa mali na kutengwa na familia.

“Wengi wao hufukuzwa nyumbani, wanaachwa bila chochote na bado wanapaswa kulea watoto. Wengine hujificha kwenye ulevi au hata kufikia hatua ya kujaribu kujiua kutokana na msongo wa mawazo,” anasema askofu huyo.

Askofu EllyJoy Moi ambaye anawainua wajane kwa kuwapa mafunzo na msaada wa kisaikolojia. PICHA|BONFACE BOGITA

Kupitia kanisa lake, Askofu Moi ameanzisha mpango wa kuwasaidia wajane, akiwapa msaada wa chakula, mavazi na hata usaidizi wa kisaikolojia.

Kila mwezi, hupokea mahitaji ya msingi kama unga, mafuta, sukari na wakati mwingine maharagwe au mchele.

Zaidi ya misaada ya kimwili, mpango huo pia unalenga uponyaji wa kihisia.

Daktari wa saikolojia, Yuvinalis Momanyi, anayeshirikiana na kanisa hilo, anasema huzuni ni mchakato unaohitaji muda na uelewa.

“Watu wengi hudhani majonzi yana mwisho wa haraka, lakini ni safari. Wajane hupitia hatua tofauti na bila msaada, wanaweza kuzama zaidi katika huzuni au hata kukataliwa na jamii,” anaeleza.

Anasema wengi wa wanaowahudumia wameachwa na familia zao na kukosa msaada, jambo linalozidisha mateso yao.

Hivi karibuni, zaidi ya wajane 80 walipata fursa ya kusafiri hadi Mombasa kwa mapumziko ya wiki moja yaliyoandaliwa na Askofu huyo iliyolenga kuwapa nafasi ya kupumzika, kufurahia maisha na kujenga upya matumaini.

“Walifurahia sana. Ilikuwa mara yao ya kwanza kutoka nje ya mazingira yao ya kawaida. Walicheka, waliogelea na walipata nafasi ya kusahau huzuni zao kwa muda,” anasema Askofu Moi.

Wito sasa unatolewa kwa serikali kuunda sera maalum za kulinda wajane, hasa katika masuala ya urithi wa mali, afya ya akili na ukuwawezesha kiuchumi.

“Tunahitaji mawakili watakaowatetea na madaktari watakaowasaidia kiafya. Serikali pia inaweza kuanzisha mipango ya kuwawezesha kiuchumi ili wasitegemee misaada kila mara,” anasisitiza.

Kwa Josephine na maelfu ya wajane wengine nchini, matumaini yao yako mikononi mwa jamii na serikali ili kuhakikisha hawabaki peke yao katika safari ya majonzi na kujijenga upya.