Habari za Kitaifa

Kenya hatarini kushindwa kulipa deni la kigeni la Sh3 trilioni, Mdhibiti Bajeti asema

Na DAVID MWERE March 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MDHIBITI wa Bajeti, Margaret Nyakang’o, ameonya kuwa serikali iko hatarini kushindwa kulipa deni la kigeni la Sh3.32 trilioni linalotarajiwa kulipwa ndani ya mwaka mmoja iwapo haitachukua hatua madhubuti za kurekebisha matumizi ya fedha za umma.

Dkt Nyakang’o alieleza kuwa mapendekezo ya kupunguza nakisi ya bajeti na deni la umma kupitia kupunguza matumizi na kuongeza mapato yamepuuzwa na maafisa wa Wizara ya Fedha.

Alionya kuwa mzigo mkubwa wa kulipa deni utapunguza uwezo wa serikali kufadhili miradi ya maendeleo na huduma muhimu kama afya, elimu na ulinzi wa jamii.

Alifichua kuwa kufikia Desemba 31, 2025, deni la umma lilikuwa limefika Sh12.3 trilioni. Serikali imelazimika kukopa zaidi, hasa katika soko la ndani, kwa gharama kubwa.

“Kiwango kikubwa cha kulipa deni kinaongeza hatari ya kifedha na shinikizo la muda mfupi,” alisema mbele ya Kamati ya Bunge ya Deni la Umma.

Aliongeza kuwa kutegemea mikopo ya muda mfupi kunaweka serikali katika hatari ya kukopa upya mara kwa mara.

Dkt Nyakang’o pia alibainisha kuwa serikali imewahi kuchelewesha ulipaji wa dhamana za thamani ya Sh53.6 bilioni, jambo linalotia shaka uwezo wake wa kulipa madeni.

Aidha, kupungua kwa thamani ya shilingi ya Kenya dhidi ya sarafu kuu za kigeni kumeongeza gharama ya kulipa deni la nje.

Wakati huo huo, Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Nancy Gathungu, ilionyesha kuwa serikali ililipa Sh6.6 bilioni kama ada ya mikopo ambayo haikutumika kati ya 2020/21 na 2023/24.

Hali hii imeathiri utoaji wa huduma muhimu kama elimu na afya, huku pia ikilemaza miradi ya maendeleo.