Raila Jnr alenga kurithi ufuasi wa babake jijini
RAILA Odinga, Jnr Mwanawe marehemu aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga ameahidi kuwa atakita siasa zake katika Kaunti ya Nairobi huku akilenga kurithi ngome za kisiasa za babake.
Raila Jnr amezitaka jamii ambazo zilikuwa msingi na mhimili wa siasa za babake zimuunge mkono anapoanza safari yake siasa.
Kwa muda sasa, Raila Jnr amekuwa akiyapokea makundi mbalimbali ya wananchi katika afisi za wakfu za Jaramogi Oginga Odinga ambako ni afisi za marehemu babake na babu yake Jaramogi Oginga Odinga.
Wiki jana aliwapokea, wakazi na makundi mbalimbali kutoka eneobunge la Kibra ambako babake aliwakilisha bungeni kwa zaidi ya miaka 20.
“Kibra ina watu ambao wanatoka makabila yote na hawafai kugawanywa kwa msingi wa kikabila. Nimewasikia na nitaanza kuwatembelea hivi karibuni,” akasema Raila Jnr, baadhi ya wakazi wakimtaka awanie ubunge wa eneo hilo.
Pia kumekuwa na wito kwamba Raila Jnr awanie ubunge wa Embakasi Kusini ambako pia amekuwa akipokelewa vyema na makundi mbalimbali ya kijamii.
“Nitashirikiana na kila mtu ikiwemo akina mama, wanaume, wanawake na watu wanaoishi na ulemavu kuhakikisha tunaimarisha maisha ya watu wetu. Sekta za afya na elimu zinachangia kujenga jamii na tutahikisha tunaimarisha sekta hizi,” akaongeza Raila Jnr.
Kiongozi huyo alisema mlango wa u wazi kwa wakazi kueleza na kushuriana na familia ya Odinga kuhusu masuala yanayowasibu.
Aidha Raila Jnr alisema sasa analenga miradi mbalimbali Kibra, Langata and Embakasi Kusini yanayolenga kuimarisha mapato ya vijana, wanawake na hata maslahi ya wakongwe.
Tayari Raila Jnr amepata uungwaji mkono baada ya kujitosa kisiasa kutoka kwa wanasiasa mbalimbali akiwemo ami yake Dkt Oburu Oginga na Naibu Gavana wa Kisumu Mathews Owili.
Dkt Oginga kwenye mahojiano na Taifa Dijitali hivi majuzi alisema kuwa Raila Jnr ana baraka zake kuwania kiti chochote cha kisiasa ambacho anataka huku akisema kama familia wanalenga kuimarisha zaidi ODM
Dkt Oginga alikuwa mwandani wa marehemu Raila na wawili hao walishirikiana kisiasa tangu kifo cha baba yao marehemu baba yao Jaramogi Oginga Odinga.
Mbunge wa Makadara ambaye pia ni mwenyekiti wa ODM jijini Nairobi, George Aladwa, amekuwa akimuunga Mbunge wa EALA Winnie Odinga ambaye ni dadake Raila Jnr kujitosa katika siasa za nchi.