Habari za Kitaifa

IEBC yapuliza kipenga cha kuchukua kadi vijana wakiambiwa ‘wakati ni sasa’

Na MOSES NYAMORI, BENSON MATHEKA March 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JUHUDI za kuimarisha usajili wa wapigakura nchini zimeshika kasi huku takwimu zikionyesha kuwa zaidi ya wapigakura milioni 5.8 wanalengwa kusajiliwa kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.

Kinachodhihirika wazi ni kuwa sehemu kubwa ya kundi hili ni vijana waliofikisha umri wa kupiga kura, jambo linaloipa kampeni yao ya ‘Niko Kadi’ uzito mkubwa katika mchakato huo.

Tume ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imeanza shughuli ya mwezi mmoja ya kusajili wapigakura kwa wingi wakati ambao vijana wanaendesha kampeni ya Niko Kadi kuhimizana kujisajili kwa uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2027.

Katika Kaunti ya Nairobi, tume hiyo inatarajia kusajili wapigakura wapya 310,486.

Jiji hili lina idadi kubwa ya vijana, wengi wao wakiwa wanafunzi, wafanyakazi wa sekta isiyo rasmi na wanaoingia soko la ajira kwa mara ya kwanza.

Hawa ndio wanaolengwa zaidi na kampeni ya Niko Kadi, inayohamasisha vijana kujitokeza na kupata kadi za kupiga kura mapema.

Kaunti ya Kakamega inafuata ikiwa na wapigakura wapya 236,156 wanaolengwa, huku Nakuru ikiwa na 221,164 na Bungoma 216,411.

Hizi ni kaunti zenye idadi kubwa ya vijana vijijini na mijini ambao bado hawajasajiliwa, na ambao wanaweza kuwa na mchango mkubwa katika kuamua mwelekeo wa siasa za taifa.

Katika Ukanda wa Pwani, Kilifi inaongoza huku IEBC ikilenga kusajili wapigakura wapya 168,131, ikifuatiwa na Kwale (102,195) na Mombasa (94,307).

Kwa miaka mingi, maeneo haya yamekumbwa na viwango vya chini vya usajili wa wapigakura miongoni mwa vijana, hali inayoweza kubadilishwa kupitia kampeni za uhamasishaji kama vile Niko Kadi.

Katika ukanda wa Mlima Kenya ambao umekuwa muhimu kisiasa, wapigakura 183,783 wanalengwa kusajiliwa Kiambu, Meru 156,592 na Murang’a 94,365, Embu 54,313 na Tharaka Nithi 38,481.

Hapa, vijana wanachukuliwa kama kundi muhimu litakaloamua iwapo ushawishi wa kisiasa utaendelea kubaki au kubadilika kuelekea 2027.

Katika Bonde la Ufa, Nakuru inaongoza huku IEBC ikilenga wapigakura wapya 221,164, Narok 147,768, Uasin Gishu 118,261, Trans Nzoia (120,037) na Nandi (101,442).

Nyanza nayo inaonyesha mwamko mkubwa, huku IEBC ikilenga wapigakura wapya 159,245 katika Kaunti ya Kisii, Homa Bay 147,809 na Migori 146,869.

Kisumu, tume hiyo inalenga kusajili wapigakura wapya 133,740 huku ikinuia kunasa 123,142 Siaya.

Kaskazini Mashariki, Mandera inaongoza, tume hiyo ikilenga kusajili wapigakura wapya 121,563, Garissa 111,542 na Wajir 107,836.

Licha ya changamoto za miundomsingi na umbali, juhudi zinaendelea kuhakikisha vijana katika maeneo haya hawabaki nyuma katika usajili wa wapigakura.

Katika ngome ya kinara wa Wiper, Kalonzo Musyoka ya Ukambani, kaunti za Machakos, Kitui na Makueni pia zimejitokeza kuwa na idadi kubwa ya wanaolengwa kusajiliwa.

IEBC Inalenga kusajili wapigakura 133,692 Machakos, Kitui 138,780 na Makueni 109,141.

Hizi ni kaunti zenye idadi kubwa ya vijana ambao kwa muda mrefu hawajashiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi.

Baadhi ya kaunti zenye idadi ndogo ya wanaolengwa ni kama Lamu (15,069), Tana River (38,564) na Samburu (39,937).

Katika Kaunti ya Laikipia tume hiyo inalenga kusajili wapigakura wapya 52,687, huku Baringo ikiwa na 82,521, Pokot Magharibi 78,479, Samburu 39,937, na Elgeyo/Marakwet 52,738.

Hizi ni kaunti zenye idadi ndogo ya wapigakura kuliko zile za mijini, lakini kwa vijana walio katika maeneo haya, usajili ni fursa muhimu ya kuweza kushiriki kikamilifu katika demokrasia ya taifa.

Tume hii inalenga wapigakura wapya 106,263 katika Kaunti ya Kajiado, Kericho 101, 881 na Bomet 105,599.

Kampeni ya Niko Kadi imejikita katika kuwahamasisha vijana kuelewa kuwa sauti yao ina nguvu kupitia kura.

Kwa mara ya kwanza katika historia ya kisasa ya uchaguzi nchini, vijana wana nafasi ya kubadilisha kwa kiasi kikubwa matokeo ya kura ikiwa watajitokeza kwa wingi kujisajili na hatimaye kupiga kura.

Hii ndiyo sababu juhudi zinaelekezwa katika kuwafikia kupitia mitandao ya kijamii na mikutano ya hadhara.

Wadau wa uchaguzi wanaonya kuwa kukosa kwa vijana kujisajili kutamaanisha kupoteza nafasi ya kushiriki katika maamuzi muhimu ya taifa.