Kenya yaungana na Uingereza, Amerika kuchunguza miwani tata
OFISI ya Kamishna wa Ulinzi wa Data (ODPC), imeanza uchunguzi kuhusu miwani tata ya Ray-Ban Meta AI kufuatia malalamishi yaliyowasilishwa na shirika la The Oversight Lab kuhusu uwezekano wa kutumika kwa miwani hiyo kufuatilia watu na kurekodi picha na video za faragha bila kibali nchini Kenya.
Katika barua iliyoandikwa Machi 31, ODPC ilisema kuwa zaidi ya mashirika na watu 150 walitia saini barua ya kuunga mkono uchunguzi huo, wakitaka pia ufanywe kwa uwazi na ushirikishaji wa umma.
Hatua hiyo inaifanya Kenya kujiunga na mataifa kama Uingereza na Amerika ambako kampuni hiyo inakabiliwa na kesi za ukiukaji wa faragha ya data.
“Ofisi ya Kamishna wa Ulinzi wa Data imethibitisha kuwa tayari imeanzisha uchunguzi kwa hiari kuhusu masuala ya faragha yanayohusiana na miwani ya Ray-Ban Meta na uchakataji wa data binafsi kwa ajili ya kufundisha Meta AI.
Matokeo yatatangazwa baada ya kukamilika kwa uchunguzi,” alisema Kamishna wa Ulinzi wa Data Kenya, Immaculate Kassait.
Mnamo Machi 6, kundi la kutetea haki za kidijitali liliandikia ODPC likitaka hatua za haraka kuhusu uwezo wa miwani hiyo kufuatilia watu na kurekodi maudhui ya faragha bila idhini.
Pia lilitaka uchunguzi kuhusu uchakataji haramu wa data kwa ajili ya mafunzo ya AI.
Mkurugenzi Mtendaji wa The Oversight Lab, Mercy Mutemi, alisema ODPC imefanya vyema kuchukua hatua, lakini akasisitiza umuhimu wa uwazi.
Alionya kuwa matumizi ya miwani hiyo yanaweza kuathiri jamii zilizo hatarini na wafanyakazi wanaochakata data.
“Kama ilivyokuwa kwa sakata la Worldcoin, Kenya inatumika kama majaribio ya teknolojia hatari za AI,” alisema.
Ripoti za wanahabari pia zimebaini kuwa data iliyokusanywa kimataifa kupitia miwani hiyo ilitumwa Nairobi, katika kampuni ya Samasource Kenya EPZ Limited, ambako wafanyakazi walipewa kazi ya kuichambua.
Wakati huo huo, nchini Uingereza, mdhibiti wa data ameibua wasiwasi kuhusu matumizi ya miwani hiyo kushughulikia maudhui muhimu.