Jamvi La Siasa

Ukuruba na Uhuru na Gachagua utakavyokuwa pigo kwa Ruto Mlima Kenya

Na JUSTUS OCHIENG, MWANGI MUIRURI April 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UKURUBA mpya wa kisiasa kati ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta na aliyekuwa naibu wa rais, Bw Rigathi Gachagua unaweza kubadilisha kabisa siasa za Mlima Kenya na kuathiri mipango ya Rais William Ruto katika uchaguzi mkuu wa 2027.

Kilichokuwa uhasama mkali kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2022 kati ya viongzo hao wawili sasa kinaonekana kubadilika kuwa makubaliano ya kisiasa yanayopangwa kwa makini, ambayo yanaweza kuunda upya mwelekeo wa kisiasa wa eneo hilo na kubadilisha nguvu za kisiasa kitaifa.

Kuonekana kwao pamoja wakati wa mazishi ya seneta wa zamani wa Kirinyaga, Daniel Karaba mnamo Jumatano, kumeelezwa na wachambuzi kama tuki linalovuka mipaka ya ishara.

Wachambuzi wanasema kwamba hatua hiyo ni matokeo ya mazungumzo ya kimya yaliyofanyika kwa miezi kadhaa nyuma ya pazia, yanayolenga kuunganisha kura za Mlima Kenya chini ya mwavuli mmoja wa kisiasa.

Mchambuzi wa kisiasa Prof Gitile Naituli alisema ushirikiano huo umekuwa ukijengwa kwa muda mrefu.

“Ushirikiano huu umekuwa ukijengwa kwa muda,” alisema, akitaja msururu wa mazungumzo ya kimya na ishara za maridhiano kuziba pengo kati ya viongozi hao wawili.

Moja ya ishara hizo ilikuwa ziara ya katibu mkuu wa zamani wa Jubilee, Jeremiah Kioni mnamo Machi 20 nyumbani kwa Gachagua, akiwa na zawadi ya mifugo, ishara ya kitamaduni ya maridhiano.

Kulingana na wachambuzi, maridhiano ya kisiasa kati ya Uhuru na Gachagua yana athari kubwa, hasa kwa Rais Ruto, ambaye alishinda kwa msaada mkubwa kutoka eneo hilo mwaka wa 2022.

Mchanganuzi wa siasa Prof Peter Kagwanja anasema muungano huu unavuruga hesabu zilizomuwezesha Ruto kupata kura nyingi eneo hilo na kushinda urais.

“Ruto alipata asilimia 87 ya kura hapa mwaka wa 2022. Kuna dalili zote kuwa sehemu kubwa ya wapigakura wamembadilisha nia,” alisema.

Ushirikiano unaojitokeza unaweza kuharibu matumaini yoyote ya Ruto kurejea katika eneo hilo, na kufanya azma yake ya kuchaguliwa kwa muhula wa pili kuwa ngumu zaidi.

Naibu Rais Kithure Kindiki ameonekana kubadilisha sauti yake katika ziara zake za Mlima Kenya, akisisitiza huduma badala ya migongano ya kisiasa.

Akizungumza alipozuru Embu na Meru, Prof Kindiki aliwataka wananchi kuungana akisema: “Bado tutaendelea kuwa jamii moja. Sijakosana na kiongozi yeyote, hata wale walionionyesha adui. Nimewasamehe bila masharti.”

Wachambuzi wanasema mabadiliko haya yanathibitisha juhudi za kupunguza mvutano katika eneo ambalo linaendelea kubadilika kisiasa.

Ushirikiano huu unaweza kulazimisha Rais Ruto kubadilisha mkakati wake kuhusu Mlima Kenya, huku ukiwapa wapinzani wake nguvu kitaifa.

Kiongozi wa chama cha Wiper, Kalonzo Musyoka, na mgombea urais wa Jubilee, Fred Matiang’i, wanaonekana kuwa sehemu ya kuunganisha viongozi hawa.

Huku Kenyatta akimpongeza Musyoka, anamtaja Matiang’i kama mgombea wa urais wa Jubilee.

Kauli za Gachagua akiwa Ukambani wiki hii zilichukuliwa kama ishara ya kumuunga Musyoka kuwa mgombea urais wa muungano wa upinzani.

Wachambuzi wanasema handisheki ya Uhuru na Gachagua ni hatua muhimu inayoweza kubadilisha ulingo wa kisiasa wa Mlima Kenya, tabia za wapigakura na mwelekeo wa Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Aliyekuwa afisa wa utawala, Joseph Kaguthi, anasema “kuungana kwa Kenyatta na Gachagua kutatupa nafasi ya kuunda Kamati ya Ukweli, Haki na Maridhiano ya eneo hili ili kuleta maridhiano kati yetu.”