Habari Mseto

Pasaka: Viongozi nchini wahimizwa wadumishe amani

Na WAANDISHI WETU April 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VIONGOZI wa kidini nchini wametoa wito wa amani na umoja huku mvutano wa kisiasa ukiongezeka kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Haya ayalijiri huku waumini wa Kikristo wakisherehekea Ijumaa Kuu kuadhimisha kifo cha Yesu Kristo.

Kote nchini waumini walikusanyika makanisani kusherehekea Pasaka wakirudia hatua zilizoelekeza Yesu Kristo kwenye mateso na kifo chake msalabani.

Askofu Mkuu wa Dayosisi Kuu la Kanisa Katoliki la Nairobi, Philip Anyolo, aliongoza ibada kupitia sehemu mbalimbali za jiji huku biashara nyingi zikibaki kufungwa.

Mratibu wa Kanisa la Holy Family Basilica, Padre Michael Ndichu, alisisitiza umuhimu wa kujitolea na huduma kwa wengine, akilinganisha mateso ya Kristo na changamoto za sasa za taifa.

“Tunahitaji kufuata mfano wa Bwana Yesu Kristo ambaye alijitolea kuokoa binadamu. Lazima tujifunze kujitolea na kuhudumia wengine,” alisema.

“Kashfa, kodi zinazoongezeka, na changamoto zingine nyingi zinabana maisha ya Wakenya. Tunapaswa kusaidiana na kuombea kila mmoja. Hata viongozi wanatakiwa kuhudumia wengine.”

Askofu wa Kanisa la Kianglikana, Jackson Ole Sapit, akihubiri katika Kanisa Kuu la All Saints, aliwahimiza waumini kushikilia imani hasa wakati nchi inapoelekea uchaguzi mwingine.

“Katika Pasaka hii, kama Yesu Kristo, tunaitwa kumuachia Mungu hofu na wasiwasi yote. Tunapaswa kumuachia yote tuliyo nayo ili atuimarishe na kutuendeleza kiimani,” alisema.

Na huko Eldoret, mamia ya waumini walijumuika chini ya uongozi wa Askofu Dominic Kimengich.

Mji mzima ulikuwa na ukimya wa kipekee huku waumini wakishiriki ibada ya kuiga mateso ya Kristo.

Katika kaunti ya Trans Nzoia, makanisa yalijaa waumini wakishiriki ibada ya Ijumaa Kuu, huku wengine wakitumia muda nyumbani na familia zao.

Katika Kanisa la AIC Nuru, Askofu Benjamin Tarus, alitumia fursa hiyo kuhimiza umoja wa kitaifa na maadili, akionya dhidi ya siasa za kikabila zinazogawanya taifa.

“Ni wakati wa kujikabidhi kwa Kristo na kutafakari kuhusu dhabihu yake. Kifo chake msalabani kinapaswa kutufundisha jinsi ya kuishi maisha mema na kushirikiana kila siku,” alisema.

Katika kaunti ya Homa Bay, viongozi wa dini walihimiza vijana kujiandikisha kama wapiga kura, wakipigia debe kampeni ya Niko Kadi, huku wakisisitiza kuwa kushiriki uchaguzi ni wajibu muhimu wa kiraia.

Askofu William Abuka alisema ubinafsi wa wapiga kura unaweza kuathiri ubora wa uongozi.

“Tunapigia kampeni Niko Kadi kwa sababu inawasaidia vijana. Hii ni fursa bora kwa vijana kujisajili,” alisema.

Katika kaunti ya Kisii, waumini walisafiri mtaani kwa tafakari ya mateso ya Kristo. Father Wilfred Oseko aliwaonya waumini kushikilia imani, kuonyesha huruma, na kuthamini zawadi ya maisha.

Huko Kisumu, Padre Fred Odhiambo aliwahimiza waumini kuwa Pasaka isiwe sherehe tu, bali pia tafakari kuhusu mafundisho ya Kristo katika maisha ya kila siku.

Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Mombasa ya Kanisa Katoliki Martin Kivuva alisisitiza jukumu la viongozi wa dini katika kuzuia vurugu za uchaguzi na kuonya dhidi ya ufisadi na kutisha wapiga kura.Viongozi wa kitaifa pia walitumia Pasaka kuhimiza umoja na amani.

Naibu Rais Kithure Kindiki alitaja kifo cha Kristo kama ishara ya upendo na ukombozi, huku Rais William Ruto akihusisha ufufuo na uvumilivu katika changamoto.

Ijumaa Kuu ni ibada inayofundisha waumini kuzingatia mateso, dhabihu, na ukombozi wa binadamu, huku ikihusisha tafakari ya changamoto binafsi na jamii.

Sherehe za mwaka huu ziliambatana na presha za kiuchumi, mabadiliko ya kisiasa, na mjadala wa kitaifa kuhusu uwajibikaji na uongozi.