Orengo anakodolea macho historia mbovu hatari ya kuwa gavana wantam ikimzonga Siaya
HUENDA historia ikajirudia kwa Gavana James Orengo wa Siaya katika uchaguzi mkuu ujao kwani dalili zaonyesha atapoteza wadhifa huo baada ya kukaidi uongozi wa chama chenye ushawishi mkubwa katika eneo hilo-ODM.
Orengo, ambaye anahudumu muhula wake wa kwanza, yuko katika mrengo wa Linda Mwananchi.
Mrengo huo unashirikisha wanachama wa ODM wanaopinga ushirikiano wa chama hicho cha chungwa na kile tawala cha UDA, chini ya Serikali Jumuishi na kuchaguliwa tena kwa Rais William Ruto.
Kwa sababu hiyo mrengo wa Linda Ground unaoongozwa na kinara wa ODM, Dkt Oburu Oginga – ambao unapigia debe kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto – umeanzisha mikakati ya kuhakikisha Gavana Orengo anapoteza katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Tayari Dkt Oginga ametangaza kwamba chama hicho kitamuunga mkono aliyekuwa Mbunge wa Rarieda, Nicholas Gumbo, kuwania ugavana wa Siaya mwaka ujao, ishara tosha kuwa uamuzi umeafikiwa ODM haitamdhamini Orengo kutetea kiti chake.
Hii ina maana kuwa endapo mwanasiasa huyo, ambaye pia ni wakili mkuu nchini, anapania kujitosa tena katika kinyang’anyiro hicho atalazimika kusaka tikiti ya chama kingine ama awe mgombeaji huru.
Kinyang’anyiro cha 2002
Hali ya kisiasa inayompata Orengo kwa sasa ni sawa na ile iliyomkumba kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2002 alipotofautiana kisiasa na marehemu Raila Odinga, kwa misingi kuwa kinara huyo wa chama cha Liberal Democratic Party (LDP) wakati huo aliamua kuunga mkono Mwai Kibaki katika kinyang’anyiro cha urais.
Orengo aliamua kuwania urais kupitia chama cha Social Democratic Party (SDP), sambamba na kiti cha ubunge cha eneo la Ugenya.
Mwanasiasa huyo alioshwa katika mikimbio ya urais akitupwa nambari tano na kura asilimia 0.4 pekee (24, 537).
Kutia msumari moto kwenye kidonda Orengo pia alibwagwa katika kura ya ubunge na Askofu Mkuu Stephen Ondiek (sasa marehemu) aliyewania kiti hicho kwa tikiti ya muungano wa NARC na kuungwa mkono na Raila.
Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa wanatahadhari kuwa Orengo atajipata pabaya 2027 endapo atadiriki kutetea kiti chake cha ugavana.
“Ni kweli kwamba Orengo alijichimbia kaburi la kisiasa alipoamua kupinga ushirikiano kati ya ODM na UDA na kujiunga na kwaya ya Wantam,” anatanguliza anasema Ambrose Weda.
“Kwa mtazamo wa wakazi wengi wa kaunti yake ya Siaya na eneo la Luo Nyanza kwa ujumla, Orengo anashabihiana kimtazamo na Rigathi Gachagua pamoja na vigogo wengine wa upinzani wanaopinga Serikali Jumuishi huku wakipanga kumtimua Rais Ruto 2027,” aeleza Weda ambaye pia ni wakili.
‘Adui’ wa manufaa ya Nyanza
Kulingana na Weda msimamo wa Orengo pia umemfanya asawiriwe kama “adui” wa manufaa ambayo Nyanza inachuma chini ya Serikali Jumuishi, ambayo inashirikisha mawaziri wawili na maafisa wengine wakuu wenye asili ya eneo hilo.
Katika uchaguzi uliopita wa ugavana 2022 Orengo alimshinda Gumbo kwa misingi kwamba aliwania kwa tikiti ya ODM huku akiungwa mkono na Raila.
Gavana huyo alizoa kura 220, 349 akifuatwa kwa umbali na Gumbo aliyepata 147,558 kwa tiketi ya chama cha UDM kinachoongozwa na Seneta Ali Roba wa Mandera.
Kulingana na Collins Ojuok udhaifu mwingine unaomponza Orengo ni kwamba anatoka katika eneobunge la Ugenya, ambalo ni mojawapo ya maeneo yenye idadi ndogo ya wapigakura Siaya.
“Kulingana na takwimu za IEBC Ugenya ina wapigakura 69,027 ikilinganishwa na maeneo kama Alego Usonga yenye wapigakura 122,002, Bondo (104,035), Gem (93,568), Rarieda (84,849) na Ugunja (60,114).
Hivyo, Orengo alishinda kwa sababu ya kuungwa mkono na Raila na pia mgombea mwenza wake William Oduol anatoka Usonga yenye idadi kubwa zaidi ya wapigakura,” anaeleza Ojuok.