Habari za Kitaifa

Kingi: PAA itashirikiana na UDA ili kuitoa pumzi ODM Pwani

Na WINNIE ATIENO April 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SPIKA wa Bunge la Seneti, Bw Amason Kingi, ameelezea wapwani sababu ya chama chake cha Pamoja African Alliance (PAA) kuamua kushirikiana na chama cha Rais William Ruto, United Democratic Alliance (UDA), katika uchaguzi mkuu wa 2027.

Bw Kingi amesema chama hicho alichokianzisha hakitasimamisha mgombea yeyote na badala yake wale wenye azma ya kuwania viti vya kisiasa wanatakiwa kutumia tiketi ya UDA.

Spika huyo alisema kwamba katika uchaguzi wa 2022, PAA na UDA ziliwasimamisha wagombea katika viti mbalimbali lakini wakashindwa baada ya ODM kuvamia ngome zake eneo la Pwani.

Hata hivyo, baada ya mazungumzo na Rais Ruto, walikubaliana kushirikiana ili kuhakikisha hawakosi viti katika uchaguzi ujao.

Kiongozi huyo alisema waliamua na Rais Ruto kutorudia makosa waliyofanya kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.

“Ganze ndiyo ilikuwa shina la chama cha PAA. Mlitupa wabunge na madiwani wengi kupitia chama chetu, ninawashukuru sana. Kwenye uchaguzi wa 2022, Bw Kenneth Tungule na wenzake walifika hapa wakiimba injili ya PAA. Mlifanya kweli na mmoja wao akaenda Bunge la Kitaifa na wengine tukawapeleka katika Bunge la Kaunti ya Kilifi,” alisema Bw Kingi.

Hata hivyo, alisema PAA na UDA ‘walifanya’ makosa na kupoteza kiti cha Magarini kwa chama cha ODM walipoamua kusimamisha wagombea tofauti kupitia vyama hivyo viwili.

Muafaka

Spika huyo alifafanua kwamba baada ya uchaguzi huo, yeye na Rais Ruto walianzisha mazungumzo ya kina.

Rais alishauri PAA kushirikiana na UDA ili kuepuka kugawanya kura na kupoteza viti, akitoa mfano wa Magarini ambapo mgombea wa ODM alishinda kwa tofauti ndogo ya kura.

“Mgombea wa UDA, Bw Stanley Karisa, alishindwa kwa kura 21 pekee. Mgombea wa PAA alipata zaidi ya kura 8,000. Tukichanganya kura hizo na za Michael Kingi ambaye aliwania kiti hicho kupitia chama cha PAA, mgombea wa ODM angeanguka. Lakini kwa sababu tuligawanya nguvu, kiti cha Magarini kikaenda kwa Azimio,” alisema Bw Kingi.

Aliongeza kuwa Rais Ruto aliwaonya kwamba wakigawanya kura tena 2027, hali ya Magarini itajirudia.

“Kwa hivyo, kuna umuhimu wa PAA na UDA kuunganisha nguvu ili tuzoe kura nyingi na viti vingi zaidi kuanzia kile cha wadi hadi cha urais,” alisema.

Hata hivyo, kabla ya kukubali kushirikiana na UDA, Bw Kingi alisema wanachama wa PAA walieleza wasiwasi wao kuhusu masuala ya Pwani kama bandari, kurejeshwa kwa mashamba, madini, kufunguliwa kwa viwanda na miradi ya maendeleo.

Alisema viongozi wa PAA walitaka hakikisho kwamba kilio cha Pwani hakitasahaulika iwapo watajiunga na UDA.

“Rais alisema kilio cha Pwani kitatiliwa maanani na UDA na kushughulikiwa vilivyo,” alisema.

Baada ya kupata hakikisho hilo, PAA iliamua kutosimamisha mgombea yeyote katika uchaguzi wa 2027.

“Wale wote waliokuwa na nia ya kugombea kupitia kwa tiketi PAA watagombea kupitia UDA. Ndiposa Mbunge wa sasa wa Ganze atagombea kupitia UDA, si PAA. Mimi nikiwa mwanzilishi wa PAA nimekubali tuingie katika chama tawala tumsaidie Rais apate muhula wa pili ili yale tuliyokubaliana yatimizwe,” alisema Bw Kingi.