Gachagua sasa aanika wosia wa kakake marehemu Nderitu baada ya majibizano na Ruto
MAELEZO mapya kuhusu wosia wa marehemu Nderitu Gachagua yameibuka baada ya kufichuliwa hadharani, yakionyesha jinsi mali yake ilivyogawanywa miongoni mwa wanufaika 23, huku pia yakibainisha mzigo mkubwa wa deni alioacha.
Kulingana na wosia uliowekwa wazi na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, wosia huo ulihusisha familia ya karibu akiwemo mama, wake wawili na watoto, pamoja na ndugu na jamaa wengine.
Mali tano ziligawanywa moja kwa moja: nyumba moja mtaani Karen ilienda kwa mke wa kwanza Margaret Nyokabi, huku nyumba mbili Karen na Nyeri zikipewa Margaret Waithegeni.
Boma la urithi (ekari nne) liligawanywa kwa wana wakubwa wa marehemu Kenneth Gachagua na Jason Kariuki kwa usawa, ilhali hisa za Mweiga Homes zilienda kwa Rigathi Gachagua.
Marehemu aliagiza mali nyingine yote kuuzwa ili kulipa deni kubwa lililofikia Sh1.07 bilioni kabla ya salio kugawanywa.
Baada ya deni kulipwa, kiasi cha takriban Sh648.8 milioni kilibaki na kugawiwa wanufaika.
Familia ya karibu ilipata asilimia 62 ya mgao huo, huku asilimia 22 ikienda kwa wanufaika wengine 14.
Asilimia 11 ilitumika kwa gharama za usimamizi na madeni mengine, na asilimia tano ikatolewa kwa wasimamizi watatu wa wosia.
Watoto wa marehemu akiwemo Susan Kirigo, Mercy Wanjira, Kenneth Gachagua na Jason Kariuki kila mmoja alipokea zaidi ya Sh64.8 milioni.
Wengine kama Eva Mukami, Margaret Nyokabi na Margaret Waithegeni walipata zaidi ya Sh32 milioni kila mmoja.
Mbali na fedha taslimu, mali nyingine kama nyumba za Lang’ata View Apartments, ploti zilizoko Nyeri na magari mbalimbali pia iligawiwa wanufaika.
Wosia huo ulisomwa Machi 11, 2017 baada ya kifo cha Nderitu mnamo Februari 24, 2017 katika hospitali ya Royal Marsden Hospital.
Kifungu muhimu cha wosia huo kilisema yeyote yule angepinga ugavi angeondolewa kabisa kwenye urithi.
Hakukuwa na pingamizi yoyote mahakamani, na Mahakama Kuu ya Kenya ilithibitisha wosia huo Machi 21, 2018.