Akili MaliMakala

Jinsi ya kulima nyasi ya Juncao

Na SAMMY WAWERU April 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JUNCAO ni teknolojia mpya ya nyasi za mifugo ambayo taifa likiikumbatia kikamilifu huenda itaipa sekta ya ufugaji Kenya afueni hasa kipindi hiki bei ya malisho inazidi kuwa ghali.

Kuwepo kwa kiangazi, ukame, magonjwa ya mimea na wadudu, vyote vikichochewa na mabadiliko ya tabianchi, wafugaji wanaendelea kutatiza pakubwa.

Uzalishaji wa maziwa, nyama, mayai na hata ngozi, bidhaa ambazo zinaingizia Kenya mapato (GDP) ikizingatiwa kuwa baadhi huuzwa nje ya nchi unaathirika na kutishia uchumi.

Ikiwa na asili ya China, nyasi ya Juncao ni mojawapo ya malisho bora yanayostahimili ukame na kutoa mavuno mengi kwa muda mfupi.

Kulingana na Profesa Lin Zhanxi wa Chuo Kikuu cha Fujian Agriculture and Forestry, China, ambaye ni mwanzilishi mtafiti, kilimo chake si kigumu, lakini kinahitaji kufuata hatua sahihi ili kupata matokeo bora.

“Kwanza, chagua eneo lenye udongo wenye rutuba na usiotuamisha maji. Ingawa Juncao inaweza kustahimili hali mbalimbali za hewa, hustawi zaidi katika maeneo yenye joto la wastani na upatikanaji wa unyevunyevu wa kutosha,” Prof Lin anasema.

Juncao iliyovunwa tayari kulishwa mifugo. Picha|Sammy Waweru

Shamba linapaswa kulimwa vizuri – kwa kulima mara mbili hadi tatu ili kulainisha udongo.

Upandaji wa Juncao hufanywa kwa kutumia vipandikizi (cuttings) badala ya mbegu. Kata vipande vya shina vyenye urefu wa sentimita 20 hadi 30 na vipandwe kwa kulaza kidogo ardhini au kwa mwinuko mdogo.

“Hakikisha kila kipandikizi kina macho (buds) kadhaa ili kuchochea ukuaji. Panda kwa nafasi ya karibu mita 1 kati ya mistari na sentimita 50 kati ya mimea,” anashauri Edwin Wekesa, Meneja Juncao Grass Technology Kenya – kampuni inayozalisha nyasi hii nchini.

Baada ya kupanda, mwagilia maji mara kwa mara hasa katika hatua za mwanzo hadi nyasi ishike mizizi vizuri. Pia, ni muhimu kuongeza samadi au mbolea ya asili ili kuboresha rutuba ya udongo na kuongeza mavuno.

Palizi ifanyike mara kwa mara ili kuondoa kwekwe au magugu yanayoweza kushindana na nyasi kwa virutubisho.

Kulingana na wakulima ambao wanakuza nyasi hii, hukua haraka, hivyo baada ya miezi miwili hadi mitatu, unaweza kuvuna mara ya kwanza.

“Baadaye, uvunaji unaweza kufanyika kila baada ya wiki sita hadi nane kulingana na usimamizi na matunzo,” anaelezea Abdirahman Ali Hassan, mfugaji kutoka Kaunti ya Wajir anayelima Juncao kupunguza gharama ya ufugaji.

Aidha, nyasi hii inaweza kukatwa na kulishwa mifugo moja kwa moja au kuhifadhiwa kama silage au hay kwa matumizi ya baadaye, hasa wakati wa kiangazi.

Edwin Wekesa, Meneja Juncao Grass Technology Kenya – kampuni inayozalisha nyasi hii nchini, akielezea kuhusu kilimo cha nyasi hii maalum. Picha|Sammy Waweru

“Huwapa mifugo wake moja kwa moja, na nyingine ninahifadhi kama hay na silage kwa minajili ya siku zijazo,” anasema Sammy Kariuki, mkulima na mfugaji wa ng’ombe wa maziwa Nakuru.

Hassan pia ni mfugaji wa ng’ombe wa maziwa na amekuwa akikuza nyasi hii ya miujiza kuanzia 2023.

Juncao ina kiwango cha protini cha asilimia 13 hadi 16 na inaweza kutoa hadi tani 240 za malisho kwa ekari chini ya usimamizi bora. Hukua hadi urefu wa mita nane na inaweza kuvunwa kila baada ya miezi miwili.

Kwa nchi kama Kenya inayokabiliwa na upungufu wa hadi asilimia 60 wa malisho ya mifugo, teknolojia ya Juncao inaweza kuwa mkombozi kwa mamilioni ya wafugaji.

Hassan na Kariuki wanaamini kukumbatia ubunifu huu, Juncao si tu nyasi—ni kinga dhidi ya ukame, chanzo cha kipato, na tumaini jipya katika enzi ya mabadiliko ya tabianchi.

Mbali na kulishwa ng’ombe na kutumika kukuza uyoga, nyasi hii pia ni mlo wa kuku, nguruwe, mbuzi, kondoo, samaki (kuunda pellets), na pia kuzuia mmomonyoko wa udongo na kasi ya upepo.

China, hutumika kuunda mavazi, soksi, mishipi, na bidhaa nyinginezo.