Kaunti yasimamisha chanjo baada ya watoto 2 walioipokea kufariki
SERIKALI ya Kaunti ya Meru imesimamisha shehena ya chanjo dhidi ya gonjwa la ukambi na huduma za utoaji chanjo katika kliniki ya kibinafsi kufuatia vifo vya watoto wawili wachanga baada ya kupokea chanjo Jumamosi.
Waziri wa Afya Meru, Dennis Mugambi alisema watoto hao wote wenye umri wa miezi tisa, waliaga dunia baada ya kupokea chanjo hiyo katika hospitali ya Rosmegg Medical Clinic, eneo la Kangeta, Igembe ya Kati.
Kulingana na Bi Belinda Gatwiri, mamake mmoja wa watoto hao, wahasiriwa walianza kuzimia mara tu baada ya chanjo.
“Mtoto wangu alikuwa wa kwanza kudungwa chanjo. Punde baada ya mtoto wangu na wa pili kudungwa, walianzwa kutetemeka. Walikimbizwa katika chumba kingine kwa matibabu. Hata hivyo, mhudumu wa afya alifunga mlango na kutuacha bila kutueleza chochote,” anasimulia Bi Gatwiri.
Anasema walilazimika kuita polisi waliowashurutisha wauguzi kuwaruhusu waingie ndani na hapo wakagundua watoto wamekufa.
Dkt Mugambi alisema japo uchunguzi umeanza, matokeo ya kwanza yanaashiria uzio wa kiwango cha juu.
“Inahuzunisha kwamba watoto walikufa baada ya chanjo. Maafisa wetu wanashirikiana na Idara ya Uchunguzi kuhusu Uhalifu (DCI) kuchunguza tukio hilo. Kwa sasa, tumesimamisha huduma zote za change katika kituo hicho. Shehena ambamo dozi hiyo ilitwaliwa imesitishwa vilevile,” alisema Dkt Mugambi, akieleza kuwa wapelelezi watachunguza vilevile uhalifu kitaaluma miongoni mwa wahudumu.