Habari za Kaunti

Ogiek waanza kusajili ardhi ya mababu zao

Na EVANS JAOLA April 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

JAMII ya Ogiek inayoishi katika eneo la Mlima Elgon katika kaunti za Trans Nzoia na Bungoma imeanza mchakato wa kusajili ekari 80,000 za ardhi yao ya jadi, baada ya kukamilika kwa mapambano ya kisheria yaliyodumu kwa miaka 22 kuhusu haki ya kuimiliki.

Wiki iliyopita, baraza la wazee wa jamii hiyo lilifanya mkutano wa siku tatu katika eneo la Chepkitale, ndani ya eneobunge la Mt Elgon ambapo walikubaliana kuanza mchakato wa kisheria wa kupata hatimiliki za ardhi hiyo.

Balozi wa Ufaransa nchini Kenya Arnaud Suquet, na ujumbe wake walipotembelea jamii ya Ogiek, katika Msitu wa Mau, 2024. Jamii hiyo imeanza kusajili ardhi ya mababu zao. Picha|John Njoroge

Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Ogiek/Ndorobo, Bw Johnson Takur, aliyeongoza mkutano huo, alisema jamii hiyo ilifikia uamuzi wa pamoja kusajili ardhi hiyo kama hatua muhimu ya kuitumia ipasavyo.

“Tumejadiliana kwa kina kama jamii na kukubaliana kwa kauli moja kusajili ardhi ya jamii na kupata hati miliki yake,” alisema mzee Takur.

Alieleza kuwa mchakato huo utasaidia jamii hiyo kusimamia rasilimali ya ardhi kwa manufaa ya muda mrefu.