Hivi UDA inadhulumu washirika wake ndani ya Serikali Jumuishi?
HATUA ya UDA kutaka kupanua mawanda yake nje ya ngome zake za kisiasa imeanza kuvuruga uhusiano wake na washirika ambao wanaona hatua hiyo kama unyanyasaji na jaribio la kuwapiga kumbo kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
ODM ililipuka hivi majuzi na kudai kuwa wanachama wake wanalazimishwa na kunyanyaswa ili kukihama chama hicho na kujiunga na UDA.
Aidha, UDA pia imekuwa na mvutano wa kisiasa na washirika wake ndani ya muungano wa Kenya Kwanza ikishinikiza vyama hivyo vivunjwe ili kujiunga nao.
Kukataa kwa baadhi ya vyama tanzu ndani ya Kenya Kwanza kujiunga na UDA kunazidisha joto la kisiasa ndani ya chama tawala.
ANC inayoongozwa na Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavadi hatimaye ilikubali kuvunjwa na kuungana na UDA mnamo Januari mwaka jana japo hatua hiyo imebatilishwa na korti.
Bw Mudavadi na uongozi wa chama hicho hata hivyo umetangaza kuwa ANC haitakuwa na wagombea kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Vivyo hivyo, PAA inayoongozwa na Spika wa Seneti Amason Kingi ilikaribia kukubali shinikizo la kuvunjwa.
Katika mkakati wa kisiasa wa kujinusuru, Bw Kingi alikataa kuvunja chama lakini akakubali kutosimamisha wagombea katika uchaguzi wa 2027.
Badala yake wataunga mkono wagombea wa UDA hasa Pwani ambacho chama hicho kina mizizi yake.
Msimamo
Hata hivyo, Ford Kenya imekataa vikali wito wa UDA wa kuvunjwa, ikisema ni hatua ya kuvuruga demokrasia na jaribio la kurejesha mfumo wa chama kimoja.
Katibu Mkuu wake, John Chikati, alisema kuwa vyama shirika vilichangia pakubwa ushindi wa serikali ya sasa, hivyo kuvitaka vivunjwe ni sawa na “kuuma kidole kilichokulisha.”
Ndani ya Serikali Jumuishi, ODM imeishutumu UDA kwa kuwashawishi wanachama wake kujiunga na chama tawala kabla ya uchaguzi ujao.
“Kuna wanachama wetu wanashawishiwa kwa pesa kujiunga na UDA. Lengo ni kuifanya ODM ionekane chama cha Luo Nyanza pekee,” alisema Kiongozi wa Wachache Bungeni Junet Mohammed.
Kwa upande wake, Mbunge wa Mwala Vincent Musau amekanusha madai hayo, akisema ni kawaida kwa chama chochote kutaka kujiimarisha kwa kusajili wanachama wengi zaidi.
Alisema mvutano unaoonekana kati ya ODM na UDA unatokana zaidi na wadhifa wa urais na chungwa kutengewa maeneo yake.
“Hatujawahi kuwanyanyasa washirika wetu, lakini ni jukumu la chama kuvutia wanachama wengi. Suala lililopo linahusu ODM kutaka wawachiwe ngome zao ilhali sisi tunaamini hilo halishabikiwi na wengi,” akasema Bw Musau.
Profesa Masibo Lumala wa Chuo Kikuu cha Moi asema vyama vidogo vimeanza kuhisi shinikizo huku muungano wa Kenya Kwanza ukilenga kuwa na chama kimoja chenye nguvu.
Anasema hatua hiyo inalenga kurahisisha siasa kwa kupunguza ushindani wa ndani na kudhibiti uteuzi wa wagombea, rasilimali na ujumbe wa kisiasa kuelekea 2027.