Siasa

Kindiki asema upinzani hauwezi kushinda 2027, kwamba Ruto ni Tutam ‘wapende wasipende’

Na GEORGE MUNENE April 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

NAIBU wa Rais Prof Kithure Kindiki ameonya upinzani akiutaka ujiandae kulambishwa sakafu katika uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.

Prof Kindiki amesema upinzani unapaswa kujiandaa kwa mchuano mkali wa kisiasa, akisisitiza kuwa hautakuwa rahisi kwao kupata ushindi kwenye kura hiyo.

“Rais William Ruto atahudumu mihula miwili, wapinzani wapende wasipende,” akasema Naibu wa Rais.

Alizungumza katika eneo la Kagumo, Kaunti ya Kirinyaga alipokuwa akikagua ujenzi wa barabara ya Kagumo–Kiamaina.

Akiwa ameandamana na Gavana wa Kirinyaga, Anne Waiguru na Mbunge wa Kirinyaga, Kati Gachoki Gitari, Naibu Rais aliwataka viongozi wa upinzani waache majitapo kuwa watashinda kwa kura nyingi.

“Ni mapema mno kuanza kujisifu, tutawaonyesha kivumbi,” akaongeza.

Seneta huyo wa zamani wa Tharaka-Nithi alisema Rais Ruto na washirika wake wako tayari kukabiliana na upinzani, aliosema umebobea kwenye siasa za matusi na propaganda badala ya kuzingatia maendeleo.

“Sisi tunaanzisha miradi ya maendeleo kwa manufaa ya Wakenya, lakini wakati wa siasa ukifika tutaonyesha kuwa sisi ni vidume vya mbegu,” akaongeza.

Aliwataka wakazi wa Mlima Kenya kutopotoshwa na vinara wa upinzani wanaowashawishi kuondoka serikalini.

“Tulichagua serikali hii na tunapaswa kubaki ndani yake ili kunufaika na rasilimali zake,” akasema.

Bw Kindiki alimkosoa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua akimtuhumu kwa kudharau viongozi wanawake waliochaguliwa katika eneo la Mlima Kenya.

“Gachagua hana heshima kwa viongozi wanawake waliochaguliwa, anapaswa kukataliwa.”

Gavana Waiguru aliunga mkono kauli hiyo, akisema wakazi wa Mlima Kenya wataendelea kuwa serikalini.

“Serikali ndiyo ina rasilimali za kujenga barabara na masoko, hatuwezi kuondoka humo,” alisema.

“Hatutaenda upinzani kwa sababu hauna cha kutoa. Mimi na Kindiki tumeungana kuhakikisha tunabaki katika uongozi wa juu kwa manufaa ya wananchi wetu,” aliongeza.

Viongozi hao wawili waliapa kushirikiana kuwarai wakazi wa Mlima Kenya kumuunga mkono Rais Ruto katika azma yake ya kuchaguliwa tena.