Faida tele kiafya za uyoga
KEVIN Mwangi Kamau ambaye ni mkuzaji wa uyoga Jijini Nairobi, anakiri familia yake kila asubuhi staftahi haikosi kitafunwa cha zao analolima.
Uyoga ni aina ya kiumbe hai kinachohesabika katika kundi la fangasi (fungi), tofauti na mimea na wanyama. Aidha, unazidi kupata umaarufu nchini Kenya na duniani kote, si tu kama chakula kitamu bali pia kama hazina ya virutubisho muhimu kwa afya ya binadamu.
Kwa muda mrefu, uyoga umechukuliwa kama mbadala wa nyama, hasa kwa watu wanaotafuta lishe bora na maisha yenye afya. “Kwenye ratiba yangu ya chakula cha asubuhi, sikosi uyoga. Mke na watoto wangu wanaupenda,” Mwangi anasema.

Barobaro huyu amekuwa akikuza uyoga tangu 2020, Kenya ilipothibitisha kuwa mwenyeji wa janga hatari la Covid-19. Kitaalamu, uyoga una kiwango cha juu cha protini, fiber na vitamini mbalimbali, hasa vitamini B zinazosaidia mwili kuzalisha nguvu. Hali kadhalika, una madini muhimu kama selenium, ambayo huimarisha kinga ya mwili na kusaidia kupambana na magonjwa sugu.
Faida nyingine kubwa ya uyoga ni uwezo wake kusaidia kudhibiti uzito. “Kwa kuwa una kalori chache na mafuta kidogo, ni chakula kinachofaa kwa watu wanaotaka kupunguza au kudhibiti uzito bila kupoteza virutubisho muhimu,” anasema Diana Mureithi, mtaalamu wa masuala ya lishe.
Aidha, uyoga husaidia kupunguza kiwango cha cholesterol mwilini, hivyo kupunguza hatari ya magonjwa ya moyo. Wataalamu wa lishe pia wanaeleza kuwa ulaji wa uyoga unaweza kusaidia kudhibiti kiwango cha sukari kwenye damu, jambo linaloufanya kuwa muhimu kwa watu wanaoishi na maradhi ya kisukari. “Vilevile, uyoga una viambato vinavyosaidia kupunguza uvimbe mwilini na kuboresha afya ya ubongo,” Diana anaelezea.

Kukabiliana na mawakala, Mwangi ameanza kuongeza thamani bidhaa zake kwa kuzichakata—akikaanga uyoga na kuongeza viungo ili kuvutia walaji wapya. Mbali na faida za kiafya, uyoga una mchango mkubwa kiuchumi. Kilimo cha uyoga hakihitaji ardhi kubwa, kinaweza kufanywa hata katika maeneo madogo mijini, na kinaanza kuzaa kwa muda mfupi.
Hii inawapa vijana na wanawake fursa nzuri ya kujiajiri na kuongeza kipato. “Ninaendeleza kilimo cha uyoga Nairobi kwenye sehemu ndogo ya ploti,” Mwangi anasema. Kilimo chake ndiyo ofisi yake ya kila siku. Hilo linafanya uyoga kuwa zao lenye faida tele, si tu katika kuboresha afya za walaji, bali pia kuinua uchumi wa nchi.