Japo tamu, kuna hatari asali kuwa na sumu, utafiti waonya
RIPOTI mpya imezua taharuki katika sekta za kilimo na afya nchini Kenya baada ya kufichua kuwa mabaki ya kemikali hatari yamepenya kwenye bidhaa za nyuki kama asali, mifumo ya maji na udongo.
Utafiti huo uliopewa wa shirika la ya Greenpeace Africa unaonya kuhusu kile ulichokiita “dhoruba kimya ya kemikali,” ambapo kemikali zinazodaiwa kulinda mazao zinaharibu msingi wa mazingira na afya ya binadamu.
Watafiti walithibitisha uwepo wa kemikali hatari sana katika bidhaa za nyuki katika kaunti za Murang’a, Kiambu na Nairobi.
Katika Murang’a, kemikali 11 tofauti ziligunduliwa, ambapo asilimia 70 zinasemekana kuwa hatari sana na asilimia 80 tayari zimepigwa marufuku katika Muungano wa Ulaya.
Kemikali inayoshambulia mfumo wa fahamu—iliyokuwa ikitumika katika kilimo kabla ya Bodi ya Kuthibiti Kemikali za Kuua Wadudu kuanza kuiondoa polepole, ilipatikana kwa wingi, mara nyingi ikizidi viwango salama. Ingawa sasa imewekewa vikwazo na hutumika zaidi kudhibiti mchwa katika ujenzi, athari zake bado zinaendelea katika mazingira.
Wataalamu wanaonya kuwa kemikali hizi huua hata nyuki au kudhoofisha mifumo yao ya kinga, uwezo wa kujielekeza na kuzaliana.
Hata kwa kiwango kidogo, zinaweza kupunguza uwezo wa nyuki kutafuta maua, kulea mabuu na kuishi.
“Kemikali hizi huchafua chakula, huharibu afya na kuua viumbe muhimu kama nyuki na viumbe vya udongo, hivyo kudhoofisha msingi wa utoshelevu wa chakula,” ilisema ripoti hiyo.
Aidha, imebainika kuwa asilimia 86 ya wakulima katika Kiambu na Nairobi hutumia kemikali angalau mara moja kwa wiki, mara nyingi wakichanganya aina tofauti.
Hali hii inaeleza kwa nini bidhaa za nyuki katika maeneo ya kilimo zina viwango vya juu vya sumu kuliko zile za maeneo ya misitu.
Maji pia yameathirika pakubwa. Katika maeneo ya Kisumu, sampuli zote za mito zilizochunguzwa zilikuwa na sumu.
Cha kushtua zaidi, uchafuzi huu umehusishwa na ongezeko la magonjwa kama kichocho na malaria. Wakati huo huo, mabuu ya mbu yanazoea kemikali hizo.