Orengo, mwanasiasa asiyezimwa na mamlaka
KATIKA historia ya siasa za Kenya, ni wachache wamejijengea sifa kwa uthabiti, ujasiri na msimamo yao kama James Orengo.
Kuanzia nyakati za ukandamizaji wa kisiasa hadi enzi ya demokrasia ya vyama vingi, Orengo amesalia kuwa sauti thabiti inayotetea haki, utawala wa sheria na kutaka uwajibikaji serikalini.
Akiwa wakili mashuhuri, Orengo alijijenga mapema kama mtetezi wa haki za raia.
Kulingana na Chama cha Wanasheria Kenya (LSK), amehusika katika kesi nyingi za kihistoria zilizolenga kulinda Katiba na kupinga matumizi mabaya ya mamlaka.
Ujasiri wake ulionekana hasa katika miaka ya 1980 na 1990 alipokuwa mstari wa mbele kupigania kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi vya kisiasa nchini.
Katika siasa, Orengo aliingia Bungeni kwa mara ya kwanza kama Mbunge wa Ugenya na baadaye akahudumu katika nyadhifa mbalimbali za serikali.
Kumbukumbu za Bunge la Taifa Kenya zinaonyesha mchango wake mkubwa katika mijadala ya kisheria na kisera, hasa kuhusu mageuzi ya katiba na utawala bora.
Baadaye, alihudumu kama Waziri katika wizara mbalimbali, akijenga sifa ya kiongozi mwenye msimamo na asiyeogopa kusema ukweli hata ndani ya serikali.
Alipochaguliwa seneta wa Siaya, Orengo aliendeleza rekodi hiyo.
Kwa mujibu wa rekodi za Seneti, alikuwa mmoja wa maseneta waliokuwa mstari wa mbele kutetea ugatuzi na haki za kaunti.
Alitumia jukwaa hilo kukosoa sera na maamuzi aliyoona yanakiuka Katiba au maslahi ya wananchi.
Leo, akiwa Gavana wa Kaunti ya Siaya, Orengo anaendeleza mapambano hayo.
Amekuwa akishinikiza uwajibikaji wa rasilimali za umma na usawa katika ugavi wa fedha kwa kaunti.
Kulingana naye, uongozi wake Siaya umejengwa juu ya misingi ya uwazi na ushirikishaji wa wananchi.
Kisiasa, Orengo ni nguzo muhimu ndani ya Orange Democratic Movement (ODM).
Baada ya kifo cha Raila Odinga, chama hicho kilikumbwa na kipindi cha mpito kilichohitaji viongozi thabiti.
Orengo alijitokeza kama mmoja wa sauti kuu ndani ya mrengo wa “Linda Mwananchi,” akisisitiza umuhimu wa kulinda haki za wananchi dhidi ya matumizi mabaya ya mamlaka.
Ujasiri wake wa kisiasa umeonekana mara kwa mara anapokosoa serikali bila woga.
Tofauti na wanasiasa wengi wanaochagua kunyamaza ili kulinda nafasi zao, Orengo amekuwa tayari kuhatarisha maslahi binafsi kwa ajili ya kile anachoamini ni haki.
Ameendelea kusisitiza kuwa demokrasia ya kweli haiwezi kuwepo bila viongozi wanaothubutu kuikosoa serikali.
Historia yake inaonyesha kuwa yeye si mwanasiasa wa maneno matupu.
Kuanzia utetezi wake mahakamani hadi mijadala yake bungeni, Orengo amejenga urithi wa vitendo.
Wataalamu wa siasa wanamtazama kama daraja kati ya enzi za mapambano ya kidemokrasia na kizazi kipya cha viongozi.
Hata hivyo, safari yake haijakosa changamoto.
Amekabiliwa na shinikizo za kisiasa, ukosoaji na wakati mwingine kutengwa.
Lakini kama historia inavyoonyesha, changamoto hizo zimezidi kumjenga badala ya kumvunja.
Kwa wengi, James Orengo anabaki kuwa mfano wa kiongozi anayethibitisha kuwa siasa zinaweza kuwa chombo cha mabadiliko chanya.
Kutoka ku wa wakili hadi mwanaharakati, waziri, seneta na sasa gavana, safari yake ni ushahidi kwamba ujasiri na msimamo vinaweza kuacha alama ya kudumu.
Katika nyakati ambapo uongozi mara nyingi hupimwa kwa umaarufu badala ya misingi, Orengo anasimama kama ukumbusho kwamba uongozi wa kweli unahitaji ujasiri wa kusema ukweli, hata pale ambapo ukweli huo haupendwi.
Orengo alipata elimu yake ya sheria katika Chuo Kikuu cha Nairobi kabla ya kuendelea na mafunzo katika Shule ya Sheria ya Kenya na ni wakili mtajika wa Mahakama Kuu.
Mwaka wa 1980, alichaguliwa kuwa Mbunge wa eneo la Ugenya kupitia chama cha KANU katika uchaguzi mdogo, na kuwa mbunge mwenye umri mdogo zaidi nchini wakati huo akiwa na miaka 29.
Alirejea tena bungeni mwaka wa 1992 ambapo alichaguliwa tena kuiwakilisha Ugenya hadi mwaka wa 1997, kisha akachaguliwa upya mwaka huo na kuhudumu hadi 2002.
Katika kipindi hicho, alijitokeza kama mmoja wa wapiganiaji wakuu wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya, akisimama kidete dhidi ya ukandamizaji wa kisiasa.
Mwaka wa 2002, Orengo alijaribu bahati yake katika kinyang’anyiro cha urais lakini hakufaulu.
Baada ya uchaguzi huo, kulikuwa na mvutano wa kisiasa kati yake na Raila Odinga, lakini tofauti hizo zilitatuliwa mwaka wa 2005 alipojiungana na chama cha Orange Democratic Movement, hatua iliyomrejesha katika siasa za kitaifa.
Katika uchaguzi wa 2007, Orengo alichaguliwa tena kuwa Mbunge wa Ugenya na kuhudumu hadi mwaka wa 2013.
Wakati wa serikali ya muungano kufuatia mzozo wa uchaguzi wa 2007, aliteuliwa kuwa Waziri wa Ardhi kuanzia mwaka wa 2008 hadi 2013.
Baada ya katiba mpya ya 2010, alichaguliwa kuwa Seneta wa Kaunti ya Siaya mwaka wa 2013 na kuhudumu hadi 2017.
Akiwa seneta, aliendelea kujijenga kama mtetezi wa haki za wananchi na usimamizi wa serikali za kaunti.