Habari

Omollo aonya wanaopanga kuvuruga mkutano wa Linda Mwananchi Kisumu

Na RUSHDIE OUDIA April 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATIBU Mkuu katika Wizara ya Usalama wa Ndani, Dkt Raymond Omollo jana alitua jijini Kisumu kwa kishindo na kutoa onyo kali kuwa serikali itapambana na magenge ya kisiasa kudumisha hali ya usalama.

Dkt Omollo aliahidi kuwa hatua kali itachukuliwa dhidi ya viongozi na makundi ya wahuni wanaolipwa kueneza ghasia na uvamizi katika eneo la Nyanza.

Ziara yake ilijiri wakati hofu imeongezeka kuhusu kurejea kwa magenge yanayofadhiliwa kisiasa, yanayolenga wapinzani, wakosoaji, kutisha wafanyabiashara na kuhatarisha amani Kisumu na kaunti jirani

Ziara ya Dkt Omollo imekuja wiki mbili tu baada ya Seneta wa Vihiga, Godfrey Osotsi, kushambuliwa mchana katika mkahawa.

Kunyoroshwa kwa Bw Osotsi kulizua ukosoaji mkali huku katibu huyo, Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen, pamoja na vyombo vya usalama vikilaumiwa kutokana na kupanda kwa uhuni wa kisiasa.

Dkt Omollo alisisitiza kuwa kila chama cha kisiasa kina haki ya kufanya mikutano popote kwa sababu Kenya demokrasia na utawala wa sheria ni msingi wa siasa zetu.

Hata hivyo, alionya kuwa uhuru huo lazima uendane na utaratibu, huku mikusanyiko ya umma na mikutano ikifuata taratibu za kisheria zilizowekwa.

“Ikiwa kuna nia ya kufanya mkutano wa hadhara, maandamano au kuwasilisha malalamishi, polisi lazima wafahamishwe mapema, na kila Mkenya yuko huru kushiriki na kukutana na wengine hadharani popote nchini, si Kisumu pekee,” akasema Dkt Omollo.

Kauli yake inajiri wakati mrengo wa “Linda Mwananchi” ndani ya ODM ukipanga kufanya mkutano wa kisiasa Kisumu wikendi ijayo (Aprili 26)
Kundi hilo, linaloongozwa na Gavana wa Siaya James Orengo, Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, limekuwa likidai kuwa kuna mipango ya kuwatumia wahuni kuvuruga mikutano yao.

Baadhi ya watu na viongozi pia walikuwa wameonya kundi hilo dhidi ya kuingia Kisumu kufanya mikutano yao. Hata hivyo, Dkt Omollo aliwahakikishia kuwa wako huru kufanya mikutano ndani ya mipaka ya sheria.

“Tunalinda haki za kila Mkenya, iwe unapigania jambo fulani, unaunga mkono au unapinga serikali. Kila mtu ana haki ya kushirikiana na umma na hakuna anayepaswa kuhisi kutishiwa wala kumtishia mwingine,” akasema Bw Omollo.

“Ikiwa unataka kufanya shughuli zako, fuata utaratibu uliowekwa. Wasiopendezwa na shughuli zako nao wanapaswa kuendelea na maisha yao bila kuingiliwa. Kama serikali, hilo ni jukumu letu.”