Habari

Imebainika kuwa pikipiki za wizi zinapitishwa mpakani na kuuzwa katika nchi jirani

Na Steve Otieno April 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WIZI wa pikipiki umegeuka kutoka uhuni wa mitaani hadi kuwa mtandao mkubwa wa uhalifu ambao unatishia moja kati ya sekta muhimu za kiuchumi nchini.
Sekta ya bodaboda huchangia Sh360 bilioni kila mwaka katika uchumi wa taifa na kuwapa riziki watu zaidi ya milioni mbili.
Lakini sekta hiyo sasa inakabiliwa na tisho kutoka mitandao ya wizi inayotumia vibaya mipaka inayoingiliwa kirahisi, mifumo dhaifu ya utekelezaji na mfumo usio rasmi wa biashara hiyo.
Kilichokuwa wizi wa kawaida, kimebadilika kuwa mtandao madhubuti unaojumuisha waendeshaji, mashirika ya fedha, wasafirishaji, fundi wa magari na makundi ya kuvuka mipaka, uchumi wa magendo unaonea kutoka mitaa ya Nairobi hadi vivuko vya mipaka mashinani.
Licha ya waendeshaji kugeukia kushiriki ujasusi, kuandikisha ripoti katika vituo vya karibu kama vile Satelaiti ya Riruta iliyo karibu na steji ya bodaboda ya Magena, na kujipanga katika vyama vya ushirika, mitandao ya wizi inakua kwa kasi.
Kwa Erick Massawe, msimamizi wa Kaunti katika shirika la Watu, moja kati ya wafadhili wakuu wa pikipiki, ni vigumu kupuuza kiwango cha kero hili.
“Wizi wa pikipiki ni tatizo kubwa siyo tu kwa wateja wetu lakini kila mhusika katika sekta hii na changamoto zinatofautiana kutegemea eneo na hali,” alisema.
Kiini cha kero hili ni mipaka ya Kenya.
Kuanzia mikondo ya Kaskazini kuingia Ethiopia na Somalia, hadi mikondo ya Magharibi kuingia Uganda na vivuko Kusini kuingia Tanzania, pikipiki zilizoibiwa hupitishwa kwa kasi na weledi. Pikipiki inapotwaliwa, saa inaanza kusonga.
Katika saa chache, inaweza kuwa nje ya nchi, isiweze kufikiwa na mamlaka ya Kenya na itahitaji polisi wa kimataifa, Interpol kuingilia kati, wanaochukua wiki au miezi kujibu, wakati ambapo pikipiki itakuwa imetoweka daima.
Kuvuka mpaka, hata hivyo, ni moja tu ya hatua za mfumo kabambe.
Ni nadra kwa pikipiki zilizoibiwa kusalia zikiwa zimeshikamana kwa muda mrefu. Baadhi huuzwa upesi kwa bei za kutupa.
Nyingine hugawanywa karibu papo hapo, na vipuri vyake kusambazwa katika masoko yasiyo rasmi, kuruhusu pikipiki husika kuingia tena sokoni kama mali halali.
“Unakuta injini zikibadlishwa kutumika kwenye meli za uvuvi,” anasema Massawe akikumbuka visa kutoka Tanzania.
“Inaashiria jinsi mtandao huu ulivyoweza kujibadilisha.”
Mtandao huo umejipanga vilivyo. Kundi moja hutambulisha na kuwalenga waendeshaji aghalabu usiku au kwenye mikondo iliyojitenga.
Jingine hushughulikia usafirishaji, kupenya vivuko rasmi na visivyo rasmi. La tatu hudhbiti uuzaji mpya, ama ikiwa mzima au vipuri.
Kila soko lina nembo zake. Ukienda Eneo la Kati, nembo kama vile Captain zinamezewa mate sana.
Aina ya TVS inapatikana sana eneo la mpakani Busia, Magharibi, huku Honda na Haujin zikibobea pwani.