Kimataifa

Papa Leo awakaripia madikteta wanaopora rasilimali asilia za Afrika

Na MASHIRIKA April 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

PAPA Leo mnamo Jumamosi alilalamikia vikali matumizi mabaya ya rasilimali asilia za Afrika, akiwakaripia “madikteta na wakandamizaji” wanaojihakikishia utajiri lakini hawatimizi ahadi zao, hivyo kusababisha mateso na vifo.

Kwenye hotuba yake nchini Angola penye utajiri wa mafuta, kituo chake cha tatu katika ziara ya mataifa manne Afrika, Papa aliwahimiza raia wa Angola kujitahidi kuwa na jamii iliyo huru kutokana na “utumwa waliotwikwa na tabaka la juu lenye utajiri mwingi lakini furaha hewa.”

Papa Leo alichukua mkondo mpya thabiti wa kuzungumza kwenye ziara yake wiki iliyopita akikabiliwa na mashambulizi kutoka kwa Rais wa Amerika, Donald Trump.

Akisafiri kwa ndege kutoka Cameroon kuelekea Angola, alijaribu kutuliza uhasama wao, akieleza wanahabari kwamba hotuba aliyotoa awali kuhusu “madikteta” haikuMlenga Trump na kwamba Papa hakuwa na nia ya kulumbana naye.

Alipotua katika jiji kuu la Luanda, Leo alilalamika kuwa “maslahi yenye nguvu yalinyakua” rasilimali asilia ya nchi hiyo iliyotawaliwa na Ureno, akirejelea bayana kampuni za kigeni zinazonufaika kutokana na sekta za mafuta, almasi na madini muhimu ya taifa hili.

“Mara nyingi watu wametazama – na wanaendelea kutazama – ardhi yenu… ili kuitwaa,” alisema Papa katika matamshi yake yaliyowasilishwa kwa Rais Joao Lourenço na viongozi wengine wa kisiasa.

“Ni mara ngapi mateso, vifo, majanga ya kijamii na kimazingira yamesababishwa na dhana hii ya uchimbaji kiasi kikubwa cha maliasili!” alisema Papa.

Papa Leo, ambaye asili yake ni Chicago, Amerika, alikuwa mtulivu kupindukia katika miezi yake ya kwanza 10 lakini katika majuma ya karibuni amezungumzia kijasiri kuhusu masuala anuwai.

Amekosoa vikali vita na ukosefu wa usawa katika ziara yake ya siku 10 barani Afrika, moja kati ya ziara ngumu zaidi kuwahi kuandaliwa papa, akitua majiji na miji 11 katika nchi nne, na kusafiri karibu kilomita 18,000 (maili 11,185) kwa zaidi ya ndege 18.

Licha ya kuwa miongoni mwa nchi zinazozalisha mafuta barani Afrika, Angola yenye idadi ya watu milioni 37 ingali inakabiliwa na ufukara uliokithiri, ambapo zaidi ya asilimia 30 ya watu wanaishi kwa chini ya Sh277.56 kwa siku, kulingana na Benki ya Dunia.

Zaidi ya nusu ya watu nchini wanajitambulisha kama Wakatoliki.

Leo alitoa wito kwa raia wa Angola “kuvunja mizunguko ya maslahi, inayopunguza uhalisia na hata maisha yenyewe, kuwa bidhaa.”

Alitoa wito kwa viongozi wa kisiasa kutilia maanani kuwasaidia watu wao wote, na sio tu maslahi ya kibiashara.

“Historia kisha itawalipizia kisasi, hata kama katika siku za majuzi baadhi huenda wakawapinga,” alisema.

Awali Jumamosi, kabla ya kuabiri ndege kuelekea Angola, Pa Leo alishiriki ibada katika jiji kuu la Cameroon, Yaounde, akiwahimiza washiriki wasipoteze matumaini licha ya changamoto zinazokabili taifa hili la Afrika ya Kati, zinazojumuisha mapigano ambayo yamewaua maelfu.

“Katika nyakati tunazoonekana kuzama, tukilemewa na nguvu zinazotushinda, wakati kila kitu kinasambaratika, Yesu yuki nasi kila wakati, mwenye nguvu kuliko nguvu zozote za giza,” Papa alieleza halaiki ambayo Vatican ilikadiria kuwa 200,000, idadi inayofanya hafla hiyo kuwa yake kubwa zaidi kufikia sasa.

“Katika kila dhoruba, anatujia na kurudia: ‘Niko hapa nawe: usiogope,” alisema.

Umati uliomsalimia Papa kwenye ziara yake Cameroon ulijawa na bashasha, wakiwemo takribani watu 120,000 waliohudhuria ibada Ijumaa, jijini Douala, wakijipanga kwenye barabara alizopitia na kuvaa mavazi yenye rangi za kuvutia zilizosheheni michoro ya sura yake.