Habari

Mkataba: Wito Rais Ruto ahakikishe wadi zote Nairobi zinapata maendeleo

Na WINNIE ONYANDO April 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

DIWANI wa Nairobi South, Waithera Chege anamshutumu Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja kwa ubaguzi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika baadhi ya wadi.

Bi Chege alimwomba Rais William Ruto kuhakikisha kuwa mgao wa fedha katika mkataba wa maendeleo wa Sh80 bilioni kati ya serikali ya kitaifa na kaunti unafanywa kwa usawa katika wadi zote 85 za jiji hilo.

Haya yanajiri huku mkataba wa maendeleo wa Sh80 bilioni kati ya serikali ya kitaifa na kaunti ukiendelea kutekelezwa baada ya kuidhinishwa mahakamani.

“Huu ni mwanzo mpya kwa Nairobi,” alisema Chege, akielezea matumaini yake kuwa hatua ya serikali ya kitaifa kushirikiana na kaunti katika utoaji wa huduma italeta mabadiliko chanya.

Kando na hayo, ametoa wito kwa Rais William Ruto kuingilia kati na kurekebisha changamoto zinazolikumba Jiji la Nairobi.

Bi Chege, pia alimkosoa vikali Gavana wa Nairobi, Johnson Sakaja, akisema ameshindwa kutimiza ahadi alizotoa wakati wa kampeni.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango wa matibabu ya magonjwa ya moyo miongoni mwa watoto katika wadi hiyo, Bi Chege alieleza kutoridhishwa kwake na uongozi wa Gavana Sakaja katika kipindi cha miaka mitatu na nusu iliyopita.

Alitaja changamoto kuu kuwa ni pamoja na usimamizi mbovu wa taka, miundombinu mbovu, pamoja na ukosefu wa maji safi na nafuu kwa wakazi wa Nairobi.