Hoja za maudhui kujibu maswali teule katika mtihani wa Insha
LEO naomba tuangazie maudhui katika maswali yafuatayo:
1) Wewe ni mtaalamu wa masuala ya kiuchumi katika Kaunti ndogo ya Inuka. Umegundua kuwa vijana wengi wanalalamika kuhusu uhaba wa nafasi za kazi.
Andika barua kwa mhariri wa Gazeti la Mvule ukipendekeza njia mwafaka ambazo vijana wanaweza kutumia kujiimarisha kiuchumi.
Baadhi za hoja:
> Vijana kuhimizwa kupata mafunzo na maarifa ya kujiinua kiuchumi.
> Jamii kuanzisha mifuko ya mikopo inayowapa vijana fursa ya kukopa pesa za kujiendeleza ama kuanzisha miradi ya maendeleo.
> Vijana kupewa mafunzo ya namna ya kudunduiza hela za kuanzisha biashara.
> Jamii kupewa vijana pembejeo/nyenzo/vivutio vya uwekezaji kama vile mbegu za kilimo/mikopo yenye riba nafuu
> Vijana kuhamasishwa kuhusu umuhimu wa kujiimarisha kiuchumi kupitia kwa mafunzo kutoka kwa waliofanikiwa kiuchumi.
> Vijana kuanzisha miradi mbalimbali ya kujiinua kiuchumi kama vile kilimo, biashara, usanii
> Vijana wenye talanta maalum kutafuta fursa ya kuzipalilia na kujichumia riziki kupitia talanta hizo.
Tanbihi: Mwanafunzi asilalamike tu bila kutoa suluhisho.
2) Umetambua kwamba baadhi ya wanafunzi shuleni mwenu wanapuuza maadili yanayofaa kuzingatiwa wakati wa kula.
Andika insha kuwaelimisha kuhusu maadili wanayopaswa kuzingatia wanapokula.
Baadhi za hoja:
> Wahakikishe wananawa mikono kabla ya kula. Kutozungumza wakiwa na chakula kinywani.
> Kutafuna chakula mdomo/kinywa kikiwa kimefungwa. Kula chakula bila pupa ili kisiwasakame.
> Kutia chakula kinywani kinachotosha ili kisiwasakame. Kutafuna chakula kikasagika kabla ya kukimeza.
> Kusafisha au kunadhifisha mahali pa maakuli.
> Kuondoa vyombo mezani ama kwenye bwalo ambavyo vilitumiwa wakati wa kula.
> Kupakua chakula ambacho ni shibe yao.
> Kumaliza chakula kilichopakuliwa ama walichokipakuwa wenyewe.
> Kutumia lugha ya adabu kuomba kitu mezani kwa mfano kama kutaka kupitishiwa chumvi.
> Kupiga foleni inavyostahili wanapoendea chakula.
> Kutorudia chakula kabla ya wenzao wote hawajapata.
> Kutokula wakiwa wamesimama.
> Kutokula wakiwa wameketi juu ya meza.
> Kutobeba chakula hadi kwenye madarasa ama kwenye mabweni
> Kutomwaga chakula mezani ama sakafuni kiholela.
> Kutotema mate wakati wa kula.
> Kutogongesha ala za kulia kama vijiko.
> Kuosha sahani ama vijiko kabla ya kuvitumia.
Kutoongea mada ya kutapisha wakati wa kula.
3) Chama cha Wanamjadala Chipukizi kimealika wanachama kwa mkutano wa pili wa mwaka.
Ajenda kuu ya kikao hiki ni kujadili mikakati ya kuimarisha uanachama kutokana na kupungua kwa idadi ya wanachama.
Miongoni mwa waliohudhuria kikao hiki ni mlezi wa chama. Ukiwa katibu wa chama hiki, andika kumbukumbu za kikao.
Baadhi za hoja
> Kuwahamasisha wanafunzi wengine kuhusu chama na shughuli zake.
> Kuwa na mijadala ya kusisimua.
> Kuwahusisha wanachama wote katika shughuli za chama.
> Kuwa na nembo ya chama.
> Kuwa na mavazi maalum ya chama.
> Kubadili uongozi wa chama.
> Kuenda ziara tofauti ili kujifunza mengi.
> Kujadili maslahi ya wanachama kama vifo, arusi, nk.
> Kupunguza ada ya kujiunga na chama.
> Kudumisha nidhamu chamani.
> Kutumia picha/michoro/mabango kunadi chama.
> Kuwaalika wageni kuja kuzungumzia masuala ya chama.
> Kutenga siku ya kunadi chama.
> Kuwa na shughuli za kuwaleta wanachama pamoja.