Utahini: Jinsi ya kujibu maswali ya muktadha
MASWALI ya muktadha hunukuu dondoo kutoka kwenye sehemu ya hadithi. Mtahiniwa huhitajika kutambua mnenaji, msemewa, mahali maongezi yanafanyika na kiini cha mazungumzo hayo.
Mnenaji anaweza kuzungumza moja kwa moja na wahusika wengine.
Huenda mhusika akajisemeza na haya hujitokeza kama mawazo yanayompitia akilini.
Katika ‘Fadhila za Punda’, Pastor Lee Imani anawazia sababu yake ya kutooa tena baada ya kifo cha mkewe.
“Nitapata wapi mwandani kama mke wangu marehemu? Hatoshi yeyote yule kujaza pengo aliloliacha mke wangu mpenzi.” (Uk.3)
Kuna miktadha mingine ambapo mwandishi ndiye hutoa maelezo kumhusu mhusika au jambo fulani.
Katika ‘Ahadi ni Deni’, mwandishi anadokeza mabadiliko yaliyotukia maishani mwa Fadhumo baada ya kufiwa na wazazi wake.
‘Huu ndio ulikuwa mwanzo wa visa na matatizo yake Fadhumo’. (Uk.66)
Msemewa anaweza kuwa mtu mmoja au kikundi cha watu. Katika ‘Nipe Nafasi’, japo ni Matweba ndiye alimuuliza Mama Kazili swali, jibu lake liliwalenga watu wote waliohudhuria kikao kilichoandaliwa kuamua kilichojuzu afanyiwe.
‘Mnahitaji niwakumbushe kuwa mimi ni raia wa Lesotho kupitia kwa ndoa? …hakuna yeyote anayeweza kunilazimisha kurudi Swaziland, hata huyo mume wangu.’ (Uk.80)
Iwapo mhusika alikuwa akijisemeza moyoni, atachukua nafasi ya msemewa. Sehemu ambako mazungumzo hufanyika huchangia vipengele tofauti.
Wahusika katika hadithi hutambulishwa katika mandhari.
Katika ‘Mzimu wa Kipwerere’, tunakutana naye Bishoo, mpenzi wake Salihina. Wahusika pia hukuzwa katika mandhari husika.
Sifa za Bishoo kama msaliti na mwongo zinajitokeza katika sehemu hii anapoeleza amemwacha mumewe akiugua kwa madai ya kumjulia hali mtoto wa jirani wao.
Mandhari husaidia hadhira kuelewa hali ya wahusika.
Katika ‘Mapambazuko ya Machweo’, watoto waliofanyishwa kazi migodini walipewa ulinzi mkali wakisimamiwa na mabawabu waliokuwa na majibwa makubwa yaliyowazuia kutoka mle.
Mandhari pia hukuza maudhui. Masuala ya ajira ya watoto na ukiukaji wa sheria yanajitokeza inapozingatiwa kuwa watoto wengine waliofanya kazi humo walikuwa chini ya umri wa miaka kumi.
Maudhui hujipenyeza katika kiini cha maongezi. Uchambuzi wa kiini hubaini tukio lililomwathi ri mhusika. Huenda maswali yanayogusia mbinu za kimtindo yakatungwa.
ZOEZI
“Ahadi ni Deni ‘Hayo ya kwenda kazini. Yapi haya nasikia mkeo anasoma? Akisoma, atasoma mpaka wapi? Mimi ninaona unamwachia tu! Kwani nani anayevaa suruali katika ile nyumba? Wewe au yeye?”
(a) Weka dondoo hili katika muktadha wake. (Alama 4)
(b) Tambua mbinu zozote mbili za kimtindo zilizotu mika kwenye dondoo hili. (Alama 2)
(c) Taja sifa mbili za msemewa. (Alama 2)
(d) Tambua na ufafanue maudhui yoyote sita yanay ojitokeza katika hadithi hii (Alama 12)